News
DCI wamtia nguvuni mshukiwa sugu Mombasa
Maafisa wa upelelezi wa makosa ya jinai nchini (DCI) wamemtia mbaroni mshukiwa mmoja katika eneo la Kazandani, kaunti ya Mombasa kwa tuhuma za matumizi yasiyofaa ya mitandao ya kijamii.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na DCI, mshukiwa huyo Halima Ngache, maarufu kama Princess Halima, amekamatwa baada ya uchunguzi kubaini kuwa anahusishwa na akaunti ya mtandao wa X, (Twitter), ambayo inadaiwa kuchapisha taarifa nyeti kuhusu mienendo ya watu wanaolindwa na serikali.
Kwa sasa, mshukiwa anazuiliwa na anaendelea kufanyiwa taratibu za kisheria kabla ya kufikishwa mahakamani.
News
Wanaume wahimizwa kuzungumzia matatizo yanayowakabili
Mwezi wa Juni huwa umetengwa kimataifa kama mwezi wa kuhamasisha jamii kuhusu afya ya akili, huku kukiwa na msisitizo maalum wa Afya ya Akili kwa Wanaume (Men’s Mental Health Awareness Month).
Mwanzilishi wa shirika la MK initiative, Millicent Khayanga alisema wanaume wengi wanakabiliwa na hali ya msongo wa mawazo hali inayofanya baadhi yao kuchukua maamuzi mabaya kama ya kujitoa uhai.
Akizungumzia suala hilo baada ya kuongoza matembezi ya kutoa hamasa kuhusu afya ya akili kwa wanaume mjini Kilifi kaunti ya Kilifi, Millicent aliishinikiza jamii kutowachukulia kama watu wadhaifu wanapopaza sauti zao kutokana na changangomoto zinazowakabili.
“Jamii imefanya wanaume kutokuzungumzia changamoto zinazowakabili kutokana na dhana kuwa mwanamume hafai kuonyesha unyonge wake,” alisema Khayanga.
Kwa upande wa wadau wengine katika mchakato huu wa kutoa hamasa kwa wanaume kuhusu afya ya akili waliishinikiza serikali kutenga fedha maalumu za kuwawezesha wanaume kujikimu kimaisha ili kuwaepusha na hali hii.

Wanaharakati wa jamii wahimiza umuhimu wa mwezi wa kuhamasisha jamii kuhusu afya ya akili
Ni kauli ambazo ziliungwa mkono na Patrick Abio mkaazi wa Kilifi ambaye alisema ikiwa jamii itawakumbatia wanaume na kutowahukumu wanapozungumzia changamoto zinazowakabili itakuwa vyema kwani hatua hiyo itadhibiti visa vya msongo wa mawazo miongoni mwao pamoja na kuzuia visa vya kujitoa uhai.
“Ikiwa serikali, mashirika na jamii zitachukulia hili kwa uzito itakuwa afueni kubwa kwa wanaume ” Alisema Abio.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Baraza la Jamii ya Sekuye lalamikia uchimbaji wa madini kiholela
Baraza la Wazee wa jamii ya Sekuye eneo la Moyale kaunti ya Marsabit limejitokeza na kulalamikia kuharibiwa kwa mazingira ya maeneo yao hasa katika kijiji cha Dabel kutokana na uchimbaji madini kiholela.
Wazee hao wamewalaumu viongozi wao ikiwemo serikali ya kaunti kwa kulinyamazia suala hilo huku wakaazi wakiendelea kunyanyaswa raslimali zao.
Baraza hilo, chini ya Katibu wake mkuu Haji Hassan Tepo, limedai kwamba uchimbaji huo wa madini kiholela, unyakuzi wa ardhi, unyanyasaji wa jamii umechangiwa na baadhi ya wawekezaji kutoka taifa Jirani la Somalia na Ethiopia ambao hawana vibali halali.
Hassan aliimtaka serikali kupitia Waziri wa madini nchini Hassan Ali Joho kuingilia kati suala hilo na kuhakikisha uchumbaji wa madini katika kijiji cha Dabel unasitishwa kwani wawekezaji zaidi ya 20 wamebuni makundi na kuendelea kuwanyanyasa wenyeji.
Hassan aliweka wazi kwamba baraza hilo pamoja na jamii ya Sekuye linapinga mpango huo na kusisitisha kwamba hawatakubali ardhi yao wanayoitegemea kwa shughuli mbalimbali kutumika vibaya.
Naibu Mwenyekiti wa baraza hilo Abdukadir Dilo alisema hali hiyo imewasabibishia hasara kwani mifugo imeangamia, uchumi wa kijiji hicho ukididimia zaidi na akamtaka rais Ruto kuingilia kati kwani licha ya Waziri Murkomen kufunga uchumbaji kufuatia utovu wa usalama bado wawekezaji kutoka Ethiopia na Somali wamekuwa wakiendeleza mpango huo.
Wazee hao hata hivyo walisisitiza kwamba hawatakubali kuachilia ardhi yao kunyakuliwa na watu wanaodai kuwa wawekezaji ilhali vijana wa eneo hilo hawana kazi, huku wanafunzi wakiacha shule na zaidi ya akina mama 22 wakiachwa na wanaume zao kufuatia suala hilo katika kijiji cha Dabel.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

