News
EACC: Wizara ya Usalama na Afya zaongoza kwa ufisadi
Utafiti mpya wa kitaifa uliofanywa na Tume ya maadili ya kupambana na ufisadi nchini EACC umeonya wakenya dhidi ya vitendo visivyo vya kimaadili na ufisadi katika Wizara ya usalama wa ndani na taasisi nyingine za umma.
Kulingana na utafiti wa mwaka 2024 wa tume hiyo, asilimia 47.8 ya wakenya waliotangamana na Wizara ya usalama wa ndani waliripoti kupitia au kushuhudia vitendo vya ufisadi au visivyo vya kimaadili.
Hali hii inaifanya Wizara hiyo kuwa na kiwango kikubwa cha matukio kama haya.
Wizara ya Afya nchini ilishika nafasi ya pili kwa asilimia 19.7, huku hazina ya kitaifa ikifuata kwa mbali kwa asilimia 5.8.
Taasisi nyingine za umma zilizojitokeza kwa wingi ni pamoja na wizara ya Ardhi kwa asilimia 5.6, uchukuzi kwa asilimia 3.9, na elimu kwa asilimia 2.6.
Utafiti huo uliofanywa kati ya Agosti na Oktoba 2024, uliwashirikisha zaidi ya watu 6,000 kote nchini na ulilenga kuelewa mitazamo na uzoefu wa wananchi kuhusiana na rushwa na maadili katika utumishi wa umma.
Ripoti hiyo ilifichua kuwa wakenya bado wanakabiliana na viwango vya juu vya hongo na tabia isiyofaa katika taasisi za umma.
Pia ilifichua hali inayotia wasiwasi ambapo rushwa inazidi kuonekana kama uovu muhimu katika kupata huduma za umma.
Ripoti hiyo pia ilibainisha kuwa wananchi wengi wanahisi wamenaswa katika mzunguko wa unyang’anyi na kuogopa kudhulumiwa ikiwa watazungumza.
Kaunti ya Nairobi iliongoza orodha ya vitengo vya ugatuzi ambapo wakaazi waliripoti kukabiliwa na visa vya juu zaidi vya ufisadi, ikifuatiwa na Kiambu, Machakos, Kisumu na Nakuru.
Tume hiyo iliwataka watumishi wa umma kuzingatia maadili ya uadilifu, uwazi na uwajibikaji katika kutoa huduma kwa Wakenya.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Rais Ruto atia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya uwekezaji wa mali
Rais William Ruto ametia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya kitaifa ya uwekezaji wa mali (Sovereign Wealth Fund), hatua inayotajwa kuwa muhimu katika juhudi za Kenya za kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kulinda utajiri wa taifa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa muda mrefu.
Utiaji huo wa saini ulifanyika katika Ikulu ya Nairobi na unaweka msingi wa kisheria wa kuanzishwa na kusimamiwa kwa mfuko wa taifa wa uwekezaji wa mali na kwamba unatarajiwa kuiwezesha nchi kuhifadhi rasilimali za umma zinazobaki baada ya matumizi ya kawaida, kufadhili uwekezaji wa kimkakati na kuimarisha uwezo wa uchumi kukabiliana na misukosuko ya kifedha siku zijazo.
Sheria hiyo mpya inaleta mfumo rasmi wa usimamizi wa utajiri wa taifa kwa kutenga akiba kwa ajili ya vizazi vijavyo, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili uwekezaji katika miundombinu ya kimkakati ili kuongeza uimara wa kifedha nchini pamoja na kuhimiza matumizi yenye uwajibikaji ya rasilimali za umma.
Mfuko huo utatumika kuwekeza mapato ya ziada yanayotokana na rasilimali za asili na mali nyingine za umma, kwa lengo la kuhakikisha manufaa yake yanawanufaisha wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
Aidha, mfuko huo unakusudia kupunguza athari za changamoto za kiuchumi kwa kutoa kinga ya kifedha wakati wa misukosuko ya uchumi.
Sheria hiyo ni sehemu ya ajenda pana ya serikali ya mageuzi ya uchumi inayolenga kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kuongeza uwazi na kuendeleza maendeleo endelevu.
Pia, sheria hiyo imeweka mfumo wa uongozi na usimamizi wa mfuko huo, ukiwemo utaratibu wa kuhakikisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi madhubuti katika uwekezaji na matumizi ya rasilimali za umma.
Maafisa wa serikali wameeleza kuwa Mfuko wa Taifa wa Uwekezaji wa Mali utakuwa na mchango mkubwa katika kufadhili miradi ya maendeleo yenye kipaumbele nchini huku ukihifadhi utajiri wa taifa kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
Kupitishwa kwa sheria hiyo kunaiweka Kenya miongoni mwa mataifa yanayoongezeka duniani ambayo yameanzisha mifuko ya taifa ya uwekezaji wa mali kwa lengo la kulinda mali za taifa, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili malengo ya maendeleo ya muda mrefu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
IEBC yakosolewa dhidi ya masharti mapya kwa wanasiasa
Kiongozi wa vijana katika Chama cha Wiper kaunti ya Kwale Nyawa Masai ameikosoa Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC kutokana na masharti mapya iliyotoa dhidi ya wanasaisa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Nyawa ameitaka Tume hiyo kuzingatia kanuni zake na taratibu za kuandaa uchaguzi na wala sio kila uchao kutoa masharti ambayo yanakinzana na majukumu ya Tume, akisema kuna taasisi zengine za umma zinafaa kuwajibika.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa katika eneo la Mwereni gatuzi dogo la Lungalunga kaunti ya Kwale, Nyawa aliesisitiza haja ya wanasiasa kupewa nafasi ya kuzungumza na wananchi sawa na kueleza sera zao bila ya vizuizi.
Kiongozi huyo wa vijana ambaye alitangaza nia yake ya kuwania kiti cha uwakilishi wadi ya Mwereni wakati wa uchaguzi ujao, amesema taifa la Kenya linazingatia demokrasia na kwamba kila taasisi inafaa kutekeleza majukumu yake.
“Katika uwaja wa siasa IEBC inakuzi moja tu kama msimamizi na kama msimamizi anaanza kutengeza sheria hapo ndipo anakosea, hii Kneya ni nchi ya demokrasia kwa hivyo IEBC isilete sheria nyingi na kufuatilia wanasiasa kuhusu pesa watatumia kwa kampeni, hiyo sio jukumu lake kuna taasisi inaitwa EACC”, alisema Nyawa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

