News
Gataya: Kaunti ya Kilifi Imeonyesha Kuwajibika Kisheria
Kamati ya utekelezaji wa sheria katika bunge la Seneti imefanya kikao na Gavana wa kaunti ya Kilifi Gedion Mung’aro kutathmini jinsi serikali ya kaunti hiyo inavyoendana na sheria za kitaifa.
Mwenyekiti wa kamati hiyo Mwenda Gataya amesema kati ya kaunti ambazo kamati hiyo imezitembelea, serikali ya kaunti ya Kilifi imeonyesha kuwajibika katika kuzingatia sheria.
Akizungumza na Wanahabari baada ya kikao hicho katika makao makuu ya Gavana wa Kilifi, Gataya ambaye pia ni Seneta wa kaunti ya Tharaka Nithi, amesema hatua hiyo imesaidia kuzuia mivutano ya kisheria.
“Tumefurahishwa na kaunti ya Kilifi jinsi ilivyofuata sheria na katiba na kama kamati ya seneti tumeridhia hatua hiyo kwamba kaunti ya Kilifi ni kati ya kaunti bora zaidi kwa kufata sheria na ndio matarajio yetu. Tumeangalia matumizi ya hazina ya wadi pamoja na zengine na kweli ni wazi kwamba imezingatia sheria kwa kuhusisha umma”, Gataya.
Kwa upande wake Gavana wa Kilifi Gedion Mung’aro amesema wanalenga kubuni sheria itakayowawezesha wasimamizi wa vijiji kutambulika kisheria, sawa na kubuni sheria itakayojumuisha wananchi katika ujenzi wa shule za Chekechea ili kudhibiti matumizi mabaya ya fedha pamoja na kubuni sheria itakayosimamia bodi ya ukusanyaji ushuru wa kaunti.

Wakati huo huo Gavana Mung’aro amedokeza kwamba tangu achukue hatamu ya uongozi, kaunti ya Kilifi imefaulu kurejesha zaidi ya shilingi bilioni 1.9 kutoka kwa kesi mbalimbali zilizowasilishwa Mahakamani, akisema ni lazima sheria izingatiwe.
“Kuna kesi moja hii kaunti ilikuwa inadaiwa milioni 926 na nikapambana hadi milioni 114, moja ilikuwa bilioni 1.1 na kuenda Mahakamani na tukashinda hiyo kesi na labda wakate rufaa na tupate taarifa kutoka Mahakamani lakini kesi hiyo tulishinda kwa hivyo kaunti imepata bilioni 1.1 pamoja na milioni 800 hiyo ni bilioni 1.9”, Mung’aro.
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

