News
Karisa Ngirani: Baadhi ya wadi Ganze zimetelekezwa na Kaunti
Mwakilishi wadi ya Ganze Karisa Ngirani anadai baadhi ya wadi ndani ya eneo bunge la Ganze zimekuwa zikitelekezwa katika maswala ya ugavi wa raslimali katika kaunti ya Kilifi.
Katika mahojiano na COCO FM, Ngirani alisema wamekuwa wakishinikiza serikali kuangazia matatizo ya wakaazi maeneo hayo ili kuhakikisha wakaazi wanafaidi miradi ya maendeleo.
Ngirani aliadai aliwasilisha hoja katika bunge la kaunti kuangazia usawa wa ugavi wa raslimali, baada ya baadhi ya wawakilishi wadi kulalamikia suala hilo.
Kulingana na mwakilishi huyo wa wadi hoja hiyo ilitupiliwa mbali licha ya kukubaliwa na wananchi baada ya kuandaa vikao vya kukusanya maoni ya umma.
“Nilikuja na hoja ambayo inaitwa “equitable bill” inaangazia usawa wa raslimali vile tunazigawanya kwa kila wadi, manake nilipoingia pale wawakilishi wengi walikuwa wanalalamika, ukiangalia ni kweli, unaangalia labda kuna mwakilishi wadi ambaye yuko karibu na gavana, huyo unapata bajeti ikitengenezwa ako na asilimia kubwa sana, lakini naskia imerejeshwa na viongozi wa juu”,alidai Ngirani
Vile vile Ngirani alidokeza kuwa suala la uhaba wa maji safi ya matumizi kwa wakaazi wa Ganze limesalia changamoto licha ya pesa zilizotengewa miradi ya maji kutolewa kwenye bajeti ya ziada.
Akiangazia masuala ya mazingira Ngirani alisema wanashirikiana na mashiriki mbali mbali kufanikisha utunzaji mazingira katika kaunti ya Kilifi, na wanapanga kuwasilisha hoja bungeni itakayotoa fursa kwa wananchi ndani ya kaunti, kutenga sehemu ya ardhi ili kuwezesha upanzi wa miti.
Alidokeza kuwa idara ya mazingira imekuwa ikitengewa mgao wa chini mno wa fedha hali ambayo imekuwa vigumu kutekeleza miradi ya kuboresha mazingira ili kukabili mabadiliko ya tabia nchi.
“Saa hii tunasukuma tuweke mswada kwamba angalau kila eneo liwe na msitu, litenge sehemu kadhaa ya ardhi ili iwe inapandwa miti iwe ni kama shamba ambalo wananchi wanawezapeana”, alisema Mwakilishi huyo wa wadi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.
News
Rais Ruto atia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya uwekezaji wa mali
Rais William Ruto ametia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya kitaifa ya uwekezaji wa mali (Sovereign Wealth Fund), hatua inayotajwa kuwa muhimu katika juhudi za Kenya za kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kulinda utajiri wa taifa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa muda mrefu.
Utiaji huo wa saini ulifanyika katika Ikulu ya Nairobi na unaweka msingi wa kisheria wa kuanzishwa na kusimamiwa kwa mfuko wa taifa wa uwekezaji wa mali na kwamba unatarajiwa kuiwezesha nchi kuhifadhi rasilimali za umma zinazobaki baada ya matumizi ya kawaida, kufadhili uwekezaji wa kimkakati na kuimarisha uwezo wa uchumi kukabiliana na misukosuko ya kifedha siku zijazo.
Sheria hiyo mpya inaleta mfumo rasmi wa usimamizi wa utajiri wa taifa kwa kutenga akiba kwa ajili ya vizazi vijavyo, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili uwekezaji katika miundombinu ya kimkakati ili kuongeza uimara wa kifedha nchini pamoja na kuhimiza matumizi yenye uwajibikaji ya rasilimali za umma.
Mfuko huo utatumika kuwekeza mapato ya ziada yanayotokana na rasilimali za asili na mali nyingine za umma, kwa lengo la kuhakikisha manufaa yake yanawanufaisha wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
Aidha, mfuko huo unakusudia kupunguza athari za changamoto za kiuchumi kwa kutoa kinga ya kifedha wakati wa misukosuko ya uchumi.
Sheria hiyo ni sehemu ya ajenda pana ya serikali ya mageuzi ya uchumi inayolenga kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kuongeza uwazi na kuendeleza maendeleo endelevu.
Pia, sheria hiyo imeweka mfumo wa uongozi na usimamizi wa mfuko huo, ukiwemo utaratibu wa kuhakikisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi madhubuti katika uwekezaji na matumizi ya rasilimali za umma.
Maafisa wa serikali wameeleza kuwa Mfuko wa Taifa wa Uwekezaji wa Mali utakuwa na mchango mkubwa katika kufadhili miradi ya maendeleo yenye kipaumbele nchini huku ukihifadhi utajiri wa taifa kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
Kupitishwa kwa sheria hiyo kunaiweka Kenya miongoni mwa mataifa yanayoongezeka duniani ambayo yameanzisha mifuko ya taifa ya uwekezaji wa mali kwa lengo la kulinda mali za taifa, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili malengo ya maendeleo ya muda mrefu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
IEBC yakosolewa dhidi ya masharti mapya kwa wanasiasa
Kiongozi wa vijana katika Chama cha Wiper kaunti ya Kwale Nyawa Masai ameikosoa Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC kutokana na masharti mapya iliyotoa dhidi ya wanasaisa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Nyawa ameitaka Tume hiyo kuzingatia kanuni zake na taratibu za kuandaa uchaguzi na wala sio kila uchao kutoa masharti ambayo yanakinzana na majukumu ya Tume, akisema kuna taasisi zengine za umma zinafaa kuwajibika.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa katika eneo la Mwereni gatuzi dogo la Lungalunga kaunti ya Kwale, Nyawa aliesisitiza haja ya wanasiasa kupewa nafasi ya kuzungumza na wananchi sawa na kueleza sera zao bila ya vizuizi.
Kiongozi huyo wa vijana ambaye alitangaza nia yake ya kuwania kiti cha uwakilishi wadi ya Mwereni wakati wa uchaguzi ujao, amesema taifa la Kenya linazingatia demokrasia na kwamba kila taasisi inafaa kutekeleza majukumu yake.
“Katika uwaja wa siasa IEBC inakuzi moja tu kama msimamizi na kama msimamizi anaanza kutengeza sheria hapo ndipo anakosea, hii Kneya ni nchi ya demokrasia kwa hivyo IEBC isilete sheria nyingi na kufuatilia wanasiasa kuhusu pesa watatumia kwa kampeni, hiyo sio jukumu lake kuna taasisi inaitwa EACC”, alisema Nyawa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

