Uncategorized
Maafisa tawala wahimiza kina mama wajawazito kujifungulia hospitali
Naibu Chifu wa eneo la Sabaki eneo bunge la Magarini kaunti ya Kilifi Rachael Malingi amewahimiza kina mama wajawazito kuhakikisha wanafika hospitalini ili kujifungua salama.
Akizungumza mjini Malindi, Malingi alisema baadhi ya kina mama ambao ni wajawazito wanaenda kwa waombezi na wakunga badala ya hospitalini hali ambayo inahatarisha maisha ya mama na mtoto aliye tumboni.
Malingi alisema vifo vya kina mama kufariki wanapojifungua nyumbani vitadhibitiwa ikiwa watatilia maanani suala la kuenda hospitalini.
‘’Ningependa kuhimiza wale wazazi ambao bado wanapata watoto tafadhalini tukaweze kupata watoto hospitalini. Hii mambo ya kuenda kwa waombezi, mambo ya kuenda kwa waganga na wewe ni mjamzito hiyo hatutaruhusu’’ alisema Malingi.
Naye Teresiah Ilobi ambaye ni mhudumu wa afya kutoka shirika la Shamiri Afrika aliwahimiza wanaume kuambatana na wenza wao wajawazito hadi kliniki ili kupata ushauri wa kitaalamu kuhusu afya ya uzazi.
‘’ Wababa muambatane na wamama kuelekea hospitalini ina umuhimu wake.Sisi kama wahudumu wa afya tunapata wakati mgumu sana wakati mama amefika na hali ya afya yake haijui’’ alisisitiza Ilobi
Ni kauli ambayo iliungwa mkono na Malingi na kusisitiza umuhimu wa wananchi kuwa na hulka ya kufika hospitalini kufanyiwa vipimo vya afya mara kwa mara.
Katika suala la usafi Malingi alisema mji wa Malindi unapaswa kusafishwa ili kudhibiti mlipuko wa magonjwa mbalimbali huku baadhi ya wakazi wakiinyooshea kidole cha lawama ofisi husika.
Taarifa ya Janet Mumbi
Uncategorized
Mshukiwa wa mauaji kuzuiliwa rumande kwa siku 7
Mahakama ya Kilifi imeagiza kuzuiliwa rumande mshukiwa wa mauaji ya Ruth Ochieng’ mwenye umri wa miaka 60 kutoka kaunti ya Kisumu baada ya mshukiwa Evans Otieno kukamatwa katika Kanisa la Newlife Prayer Center lililoko eneo la Mavueni kaunti ya Kilifi.
Otieno alitiwa nguvuni na maafisa wa usalama alipokiri kwamba alitekeleza mauaji hayo mbele ya Mchungaji wa Kanisa hilo Ezekiel Odero, akitaka aombewe kama hatua moja wapo ya kutubu dhambi zake.
Hakimu wa Mahakama ya Kilifi Charles Obulutsa amesema Otieno atazuiliwa rumande kwa siku 7 ili kumuwezesha afisa wa polisi wa kituo cha polisi cha Seme mjini Kisumu anayechunguza kesi hiyo kufika Mahakamani.
Hakimu Obulutsa, ameeleza Mahakama kwamba wakati afisa huyo wa Polisi atakapofika katika Mahakama ya Kilifi atapewa idhini ya kumchukua mshukiwa ili afunguliwe mashtaka ya mauaji mjini Kisumu.
Awali Mahakama ilielezwa kwamba mwili wa mahehemu ulipatikana na kuthibitishwa kwamba alikuwa amenyongwa na uchunguzi zaidi ulikuwa unaendelea kabla ya mshukiwa kukamatwa katika maeneo ya Kanisa la Newlife Prayer Centre, eneo la Mavueni kaunti ya Kilifi.
Kesi hiyo itatajwa tena Februari 11 katika ili kuwakabidhi maafisa wa Polisi kutoka kaunti ya Kisumu mshtakiwa huyo.
Taarifa ya Teclar Yeri
Uncategorized
Wakenya wanaopata mshahara wa chini ya elfu 30 kuondolewa PAYE
Waziri wa Fedha nchini John Mbadi amesema serikali inalenga kuwaondolea ushuru wa PAYE wakenya wanaopata mshahara wa chini ya shilingi elfu 30 kwa mwezi huku wale wanaopata mshahara wa shilingi elfu 30 hadi laki tano wakitozwa ushuru wa asilimia 25.
Waziri Mbadi alisema hatua hiyo inalenga zaidi ya wakenya milioni 1.5 na hivi karibuni atawasilisha mswada bungeni ili pendekezo hilo liangaziwe na sheria ya ushuru ifanyiwe marekebisho kabla ya kupitishwa kwa mswada wa fedha wa mwaka wa 2026.
Waziri Mbali aliyasema hayo wakati wa kikao cha kukusanya maoni ya umma katika kaunti ya Meru ambapo alikuwa amefanya kikao cha mazungumzo na Rais William Ruto na kuafikiana kuhusu pendekezo hilo.
Waziri huyo wa fedha nchini aliongeza kwamba mswada huo pia utajumuisha pendekezo la kupunguza ushuru wa PAYE kwa asilimia 5 kwa wakenya wanaopokea mshahara wa kati ya shilingi elfu 32,050 kwa mwezi hadi shilingi laki tano, akisema punguzo hilo la asilimia 5 litasaidia wakenya kumudu gharama ya maisha.
“Tumekubaliana na Rais kwamba wananchi wenye kipato cha chini wanapaswa kupata nafuu kwenye mishahra yao kwani idadi kubwa ya wananchi wanapitia hali ngumu ya maisha na hatua hii itasaidia wakenya wengi kuwa na pesa mfukoni. Sidhani kama kuna mbunge yeyote atapinga pendekezo hilo”, alisema Mbadi.
Waziri huyo wa fedha alishikilia kwamba hatua hiyo inalenga kupunguza mzingo wa ushuru kwa wakenya wa kipato cha chini na cha kati na kuwasaidia kujikimu katika kipindi hiki cha gharama ya juu ya maisha.
Kwa sasa kikomo cha ushuru wa PAYE kinaathiri wakenya wengi wenye kupokea mshahara wa kuanzia shilingi elfu 24, akisema wataalamu wamebaini kwamba kupunguzwa kwa ushuru kutachangia matumizi ya nyumbani kuwa ya usawa na kusaidia kuimarisha uchumi unaokabiliwa na mahitaji duni.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

