News
Mahakama ya Kilifi yaagiza mshukiwa wa mauaji kuzuiliwa kwa siku 21
Mahakama ya Kilifi imeagiza kuzuiliwa rumande kwa siku 21 mwanamke mmoja anayekabiliwa na shtaka la kumuuwa mwanawe kwa kumzika akiwa hai.
Hakimu wa Mahakama hiyo Charles Obulutsa ametoa agizo hilo baada ya upande wa mashtaka kuiomba Mahakama kumpa muda zaidi ili kuwawezesha maafisa wa upelelezi wa kesi hiyo kukamilisha uchunguzi wao.
Kulingana na upande wa mashtaka ukiongozwa na Nancy Njeru ulieleza Mahakama kwamba mtoto huyo alikuwa ameishi siku mbili baada ya kuzuiliwa.
Mahakama imeelezwa zaidi kwamba kabla ya mshukiwa kumzika mtoto huyo akiwa hai, ni lazima mwanamke huyo alikuwa na tatizo ndiposa upande wa mashtaka uanitaji muda zaidi kwa kufanya uchunguzi sawa na kumhoji mshukiwa.
Mshukiwa Maua Karisa anadaiwa kumzaa mwanawe tarehe 24 Mei 2026, na kutekeleza kitendo hicho tarehe 26 Mei 2026 katika eneo la Matsangoni kaunti ya Kilifi.
Kesi hiyo itatajwa tarehe 22 mwezi Juni mwaka huu.
Taarifa ya Tecla Yeri
News
Pengo katika uhamasishaji wa afya ya uzazi kilifi
Idadi kubwa ya wanawake na wasichana katika kaunti ya Kilifi bado hawajahamasishwa vilivyo kuhusu masuala ya afya ya uzazi na haki yao ya kupata huduma bora ya afya hasa katika maeneo ya mashinani.
Katika kikao ambacho kiliongozwa na shirika la Timiza Youth Initiative kwenye ukumbi wa Kibaoni mjini Kilifi kaunti ya Kilifi na kuhudhuriwa na vijana, wahudumu wa afya na wadau mbalimbali, ilibainika kuwa afya ya wanawake haijakumbatiwa vilivyo katika jamii hali ambayo imekuwa ikifanya wengi wao kupitia changamoto nyingi na hata kufariki dunia wakati wa ujauzito na wanapojifungua.
Akizungumzia hilo Brian Mundia ambaye ni mwenyekiti wa shirika hilo alisema wasichana wenye umri mdogo pia hawajaelimishwa vya kutosha kuhusu athari ya kupanga uzazi na kuavya mimba.
Mundia pia alisema vijana wengi wanaogopa kufika katika vituo vya afya kupata ushauri kutokana na hali ya unyanyapaa .
Kwa upande wake Doris Waithira Mzee wa kijiji eneo la Mnarani na ambaye pia anatoa ushauri nasaha kwa wanarika alisema akina mama wengi hawaendi hospitalini kujifungua hali ambayo pia huwa inahatarisha afya ya mtoto.
Kwa pamoja walieleza changamoto zilizopo katika kuwafikia wanawake walioko mashinani ili kutoa hamasa na kutoa wito kwa mashirika na serikali kupitia idara ya afya kushirikiana ili kuhakikisha masuala ya afya ya uzazi na afya ya mama katika jamii inakumbatiwa vilivyo.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mkasa wa moto katika shule ya Utumishi Girls Academy wasababisha vifo 16
Serikali imethibitisha kwamba wanafunzi 16 wa shule ya upili ya wasichana ya Utumishi Girls Academy eneo la Gilgil kaunti ya Nakuru wameaga dunia na wengini 79 wakajeruhiwa kufuatia mkasa wa moto ulitokea katika shule hiyo.
Waziri wa Elimu nchini Julius Migos amesema shule hiyo ilikuwa na wanafunzi 808 wakati wa mkasa huo wa usiku wa kuamkia siku ya Alhamis 28, Mei 2026, ambapo bweni moja la wanafunzi wa shule hiyo lilishika moto na kuteketea.
Akizungumza na Wanahabari baada ya kutembelea shule hiyo, Waziri Migos alisema kati ya wanafunzi 79 waliyopata majeraha na kukimbizwa hospitalini, 71 kati yao walipokea matibabu na kuruhusiwa kuondoka na wazazi wao, wanafunzi wengine 7 wakiendelea kulazwa hospitalini.
Migos hata hivyo ameonya kuchukuliwa kwa hatua kali za kisheria kwa mtu yeyote atakayepatikana amehusika katika mkasa huo wa moto kwenye shule hiyo ya Utumishi Girls Academy huku akiagiza kufungwa kwa shule hiyo kwa muda.
“Ningependa kusema kwamba sote tunajua kwamba mkasa huu umesababishwa na moto lakini uchunguzi ukikamilika na tubaini kwamba kuna watu walihusika iwe ni wanafunzi ama mtu binafsi serikali itamchukulia hatua kali zaidi”, alisema Migos
Naye Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen aliwataka wananchi kuwa utulivu na kuepuka kusambaza taarifa zisizo na uhakika mitandaoni kwani maafisa wa usalama bado wanaendelea na uchunguzi.
“Tunawataka wakenya wawe watulivu wakati uchunguzi ukiendelea na tutaeleza kila kitu baada ya kupata taarifa kamilifu kutoka kwa maafisa wetu wa upelelezi lakini sio vizuri kuweka mambo kwa mitandao na haujapata taarifa kamili,”alisema Murkomen.
Hata hivyo wazazi waliyofika katika shule hiyo wamependezeka mabweni yote katika shule mbalimbali nchini kuweka madirisha makubwa na milango mingi ili kuokoa maisha ya wanafunzi wakati wa mikasa ya moto sawa na sheria zilizowekwa na serikali kuhakikisha zinatekelezwa kikamilifu.
Maafisa wa Idara ya upelelezi wa jinai nchini DCI wamesema tayari wameanzisha uchunguzi ili kubaini chanzo cha mkasa huo wa moto katika shule hiyo ya upili ya wasichana ya Utumishi Girls Academy huko Gilgil kaunti ya Nakuru.

