News
Mkasa wa moto katika shule ya Utumishi Girls Academy wasababisha vifo 16
Serikali imethibitisha kwamba wanafunzi 16 wa shule ya upili ya wasichana ya Utumishi Girls Academy eneo la Gilgil kaunti ya Nakuru wameaga dunia na wengini 79 wakajeruhiwa kufuatia mkasa wa moto ulitokea katika shule hiyo.
Waziri wa Elimu nchini Julius Migos amesema shule hiyo ilikuwa na wanafunzi 808 wakati wa mkasa huo wa usiku wa kuamkia siku ya Alhamis 28, Mei 2026, ambapo bweni moja la wanafunzi wa shule hiyo lilishika moto na kuteketea.
Akizungumza na Wanahabari baada ya kutembelea shule hiyo, Waziri Migos alisema kati ya wanafunzi 79 waliyopata majeraha na kukimbizwa hospitalini, 71 kati yao walipokea matibabu na kuruhusiwa kuondoka na wazazi wao, wanafunzi wengine 7 wakiendelea kulazwa hospitalini.
Migos hata hivyo ameonya kuchukuliwa kwa hatua kali za kisheria kwa mtu yeyote atakayepatikana amehusika katika mkasa huo wa moto kwenye shule hiyo ya Utumishi Girls Academy huku akiagiza kufungwa kwa shule hiyo kwa muda.
“Ningependa kusema kwamba sote tunajua kwamba mkasa huu umesababishwa na moto lakini uchunguzi ukikamilika na tubaini kwamba kuna watu walihusika iwe ni wanafunzi ama mtu binafsi serikali itamchukulia hatua kali zaidi”, alisema Migos
Naye Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen aliwataka wananchi kuwa utulivu na kuepuka kusambaza taarifa zisizo na uhakika mitandaoni kwani maafisa wa usalama bado wanaendelea na uchunguzi.
“Tunawataka wakenya wawe watulivu wakati uchunguzi ukiendelea na tutaeleza kila kitu baada ya kupata taarifa kamilifu kutoka kwa maafisa wetu wa upelelezi lakini sio vizuri kuweka mambo kwa mitandao na haujapata taarifa kamili,”alisema Murkomen.
Hata hivyo wazazi waliyofika katika shule hiyo wamependezeka mabweni yote katika shule mbalimbali nchini kuweka madirisha makubwa na milango mingi ili kuokoa maisha ya wanafunzi wakati wa mikasa ya moto sawa na sheria zilizowekwa na serikali kuhakikisha zinatekelezwa kikamilifu.
Maafisa wa Idara ya upelelezi wa jinai nchini DCI wamesema tayari wameanzisha uchunguzi ili kubaini chanzo cha mkasa huo wa moto katika shule hiyo ya upili ya wasichana ya Utumishi Girls Academy huko Gilgil kaunti ya Nakuru.
News
Mbunge wa Nyali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila
Mbunge wa Nyali kaunti ya Mombasa Mohamed Ali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila kwenye kaunti hiyo, akisema anafanya siasa zake bila kujali dini, kabila au hata eneo.
Akizungumza huko Nyali, Ali alisema kuna baadhi ya viongozi katika kaunti ya Mombasa, ambao wamekuwa wakiendekeza propaganda za kumhusisha na siasa za migawanyiko ili kumharibia jina taifa linapojiandaa kwa uchaguzi mkuu ujao wa 2027.
Ali ambaye alitangaza kuwania wadhifa wa ugavana kaunti ya Mombasa, aliwataka viongozi kufanya siasa zao kwa kunadi sera zao kwa wakaazi na maendeleo ambayo watatekeleza na sio kutumia suala la ukabila kuwachafulia wengine jina.
“2017 hakuna mtu aliniita mkabila, 2022 hakuna mtu aliniita mkabila, 2027 wanasema Mohamed Ali ni mkabila.Mimi Mohamed Ali, mimi nauliza nikisimama hapa juu ya gari, niseme kabila zote za Kenya wanaweza pewa nafasi ya ugavana ni kuna makosa?,basi sasa wanazunguka wakisema Mohamed ni mkabila kwasababu ameanza kufungua watu macho’’ alisema Ali.
Aidha, Ali alisema ataendelea kuzuru maeneo mbalimbali ya kauti ya Mombasa kunadi sera zake na kuwataka wakaazi wa kaunti hiyo kuwachagua viongozi wanaofaa ambao wataimarisha kaunti hiyo kimaendeleo.
‘’Mimi nimewaambia nitatembea hii Mombasa kwa uwezo wake mwenyezi mungu kutetea wananchi wa Mombasa’’ aliongeza Ali
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Wakimbizi nusu milioni wakabiliwa na baa la njaa, Dadaab
Ripoti iliyotolewa hivi karibu na Shirika la Chakula duniani WFP ilionyesha kwamba zaidi ya wakimbizi nusu milioni wanaoishi katika kambi za wakimbizi za Kakuma na Dadaab zilizoko nchini Kenya, wako katika hatari ya kuangamia kutokana na baa la njaa.
Kambi hizi ambazo zinahifadhi wakimbizi wengi zaidi kutoka nchini Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Somalia, ziko hatari iwapo zitakosa misaada ya chakula.
Kufuatia hali hiyo ambayo pia imechangiwa na mashirika ya kimataifa kusitisha ufadhili, sasa hali huenda ikawa tofauti baada ya taifa la Korea kwa ushirikiano na Kenya kutoa ufadhili wa shehena ya nafaka ya zaidi ya tani elfu 10 ambayo inakadiriwa kuwa kima cha shilingi milioni 1.2.
Katibu katika Idara ya uhamiaji nchini Belio Kipsang, aliyepokea msaada huo wa Chakula mjini Mombasa na kuhifadhiwa katika maghala ya Shirika la WFP, ameonya kwamba iwapo Kenya itakosa kupokea msaada kutoka kwa washirika na wafadhili wengine, basi italazimika kuchukua maamuzi magumu, ikiwemo kuwaondoa baadhi ya wakimbizi.
“Nyuma ya kila takwimu kuna familia ambazo ustahimilivu wao unaendelea kujaribiwa kila siku: akina mama wanaokosa kula ili watoto wao wapate chakula, watu walio katika mazingira hatarishi wakiruka milo, na vijana wanaokabiliwa na mustakabali usio na uhakika. Hizi si takwimu za kufikirika. Zinawakilisha watu halisi ambao heshima yao, afya yao na matarajio yao ya maisha yanategemea maamuzi tunayofanya kwa pamoja,” alisema.
Wakati wa hafla hiyo ya kupokea msaada huo wa chakula kwa wakimbizi wa Kakuma na Dadaab, Mkurugenzi wa Shirika la WFP nchini Kenya Betty Ka, alisema shehena ya nafaka itasaidia kuwahudumia takribani wakimbizi nusu milioni katika miezi ijayo.
“Usafirishaji huu unaonyesha umuhimu wa ushirikiano imara katika mnyororo wa ugavi wa misaada ya kibinadamu, ambapo ushirikiano huu kati ya Kenya, Mamlaka ya bandari Kenya (KPA), Shirika la viwango la Kenya(KEBS) na mpango wa Chakula Duniani (WFP) kwa kuhakikisha kwamba chakula cha msaada kinafanikishwa”,alisema Betty.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

