News
Ofisi za Shule ya Wavulana ya Kinango zimeteketea
Baadhi ya ofisi za Shule ya Wavulana ya Kinango kaunti ya Kwale zimeteketea baada ya moto kuzuka katika shuleni hiyo usiku wa kuamkia siku ya Jumatano.
Mwalimu mkuu wa shule hiyo Siasa Mwafungo alieleza kwamba licha ya chanzo cha moto huo bado hakijabainika huenda baadhi ya wanafunzi waliotaka kwenda kwa likizo ya sikukuu ya Eid-Ul-Adha walihusika katika mkasa huo.
Mwafun go alisema kwamba moto huo uliweza kudhibitiwa japo kiasi cha mali ya thamani ya pesa imeteketea ikiwemo vitabu na vifaa vingine wanavyotumia walimu kufanya kazi zao.
“Bado tunachunguza chanzo cha moto huo lakini kiasi cha mali ya thamani ya shule imepotea kufuatia mkasa huu wa moto, maafisa wa polisi watatueleza zaidi baada ya uchunguzi kukamilika”, alisema Mwalimu mkuu.
Mwalimu huyo mkuu aliwaonya wanafunzi kwamba yeyote atakayepatikana kuhusika na mkasa huo basi hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi yake ili iwe funzo kwa wanafunzi wengine wenye utovu wa nidhamu.
“Wanafunzi tumewaonya kwamba iwapo tutabaini kwamba wamehusika katika mkasa huu basi sheria lazima itachukua mkondo wake”, alisema Mwafungo.
Wakati huo huo aliwataka wazazi wa shule hiyo kutoa shaka kwani usalama wa wanafunzi umeimarishwa huku maafisa wa upelelezi wa jinai nchini DCI katika eneo bunge la Kinango wakifanya jitihada za kubaini chanzo cha moto huo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

