News
Rais Ruto atia saini Miswada miwili kupiga jeki Mgao wa Serikali za Kaunti
Rais William Ruto ametia saini na kuwa sheria miswaada miwili muhimu inayokusudiwa kupiga jeki ufadhili wa Serikali za Ugatuzi nchini.
Rais Ruto ambaye anahudhuria Kongamano la Ugatuzi mwaka huu katika kaunti ya Homa Bay, ametia saini mswada kuhusu Ugavi wa pato la serikali kwa hazina za Kaunti wa 2025, na pia Mswada mwengine unaotoa muongozo wa matumizi ya fedha za serikali za Kaunti wa 2023.
Mswaada unaohusu usimamizi na muongozo wa matumizi ya pesa za kaunti sasa umefutiliwa mbali na kubuni Hazina ya mabunge ya Kaunti zote 47.
Mswaada huo wa nyongeza ya pato kwa kaunti umeongoza kiwango cha hapo awali kutoka Shilingi billioni 387.4 mwaka uliopita hadi kiwango cha Shilingi bilioni 415 katika kipindi cha mwaka huu 2025/26 cha matumizi ya pesa serikalini.
Hafla hiyo ya kutia saini miswaada hiyo miwili,imefanyika katika Ikulu ndogo kaunti ya Homabay Jumatano Agostu 13 2025.
Mswaada huo uliowasilishwa bungeni na Senta wa Meru Kathuri Murungi, unayapa uhuru zaidi Mabunge ya Kaunti katika masuala ya usimamizi wa fedha zao.

Hatua hiyo imetokea wakati Kongamano la Ugatuzi limefunguliwa rasmi katika Kaunti ya Homabay, kutathmini mafanikio na changamoto kwa serikali za Kaunti.
Kongamano hilo linahudhuriwa miongoni mwa wengine Wafanyi biashara na washika Dau mbali mbali wa kimaendeleo katika ngazi za Kaunti.
Hazina kuu ya Serikali sasa inatarajiwa kuhakikisha kuwa mgao huo wa fedha unafikia hazina za serikali za Kuanti kabla ya tarehe 15 ya kila mwezi
Katika muda wa miaka miwili iliyopita serikali kuu ya kitaifa imeshtumiwa vikali na Baraza la Magavana, kwa madai ya njama za kuhujumu Ugatuzi nchini.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Rais Ruto atia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya uwekezaji wa mali
Rais William Ruto ametia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya kitaifa ya uwekezaji wa mali (Sovereign Wealth Fund), hatua inayotajwa kuwa muhimu katika juhudi za Kenya za kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kulinda utajiri wa taifa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa muda mrefu.
Utiaji huo wa saini ulifanyika katika Ikulu ya Nairobi na unaweka msingi wa kisheria wa kuanzishwa na kusimamiwa kwa mfuko wa taifa wa uwekezaji wa mali na kwamba unatarajiwa kuiwezesha nchi kuhifadhi rasilimali za umma zinazobaki baada ya matumizi ya kawaida, kufadhili uwekezaji wa kimkakati na kuimarisha uwezo wa uchumi kukabiliana na misukosuko ya kifedha siku zijazo.
Sheria hiyo mpya inaleta mfumo rasmi wa usimamizi wa utajiri wa taifa kwa kutenga akiba kwa ajili ya vizazi vijavyo, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili uwekezaji katika miundombinu ya kimkakati ili kuongeza uimara wa kifedha nchini pamoja na kuhimiza matumizi yenye uwajibikaji ya rasilimali za umma.
Mfuko huo utatumika kuwekeza mapato ya ziada yanayotokana na rasilimali za asili na mali nyingine za umma, kwa lengo la kuhakikisha manufaa yake yanawanufaisha wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
Aidha, mfuko huo unakusudia kupunguza athari za changamoto za kiuchumi kwa kutoa kinga ya kifedha wakati wa misukosuko ya uchumi.
Sheria hiyo ni sehemu ya ajenda pana ya serikali ya mageuzi ya uchumi inayolenga kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kuongeza uwazi na kuendeleza maendeleo endelevu.
Pia, sheria hiyo imeweka mfumo wa uongozi na usimamizi wa mfuko huo, ukiwemo utaratibu wa kuhakikisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi madhubuti katika uwekezaji na matumizi ya rasilimali za umma.
Maafisa wa serikali wameeleza kuwa Mfuko wa Taifa wa Uwekezaji wa Mali utakuwa na mchango mkubwa katika kufadhili miradi ya maendeleo yenye kipaumbele nchini huku ukihifadhi utajiri wa taifa kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
Kupitishwa kwa sheria hiyo kunaiweka Kenya miongoni mwa mataifa yanayoongezeka duniani ambayo yameanzisha mifuko ya taifa ya uwekezaji wa mali kwa lengo la kulinda mali za taifa, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili malengo ya maendeleo ya muda mrefu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
IEBC yakosolewa dhidi ya masharti mapya kwa wanasiasa
Kiongozi wa vijana katika Chama cha Wiper kaunti ya Kwale Nyawa Masai ameikosoa Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC kutokana na masharti mapya iliyotoa dhidi ya wanasaisa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Nyawa ameitaka Tume hiyo kuzingatia kanuni zake na taratibu za kuandaa uchaguzi na wala sio kila uchao kutoa masharti ambayo yanakinzana na majukumu ya Tume, akisema kuna taasisi zengine za umma zinafaa kuwajibika.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa katika eneo la Mwereni gatuzi dogo la Lungalunga kaunti ya Kwale, Nyawa aliesisitiza haja ya wanasiasa kupewa nafasi ya kuzungumza na wananchi sawa na kueleza sera zao bila ya vizuizi.
Kiongozi huyo wa vijana ambaye alitangaza nia yake ya kuwania kiti cha uwakilishi wadi ya Mwereni wakati wa uchaguzi ujao, amesema taifa la Kenya linazingatia demokrasia na kwamba kila taasisi inafaa kutekeleza majukumu yake.
“Katika uwaja wa siasa IEBC inakuzi moja tu kama msimamizi na kama msimamizi anaanza kutengeza sheria hapo ndipo anakosea, hii Kneya ni nchi ya demokrasia kwa hivyo IEBC isilete sheria nyingi na kufuatilia wanasiasa kuhusu pesa watatumia kwa kampeni, hiyo sio jukumu lake kuna taasisi inaitwa EACC”, alisema Nyawa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

