News
Watu 12 wahofiwa kufariki baada ya ndege kuanguka Kwale
Watu 12 wanahofiwa kufariki baada ya ndege ndogo ya utalii kuanguka katika eneo la Tsimba gatuzi dogo la Matuga kaunti ya Kwale.
Ndege hiyo ilikuwa imetokea eneo la Diani kuelekea Kichwa Tembo kwa shughuli za kiutalii katika eneo la Masai Mara kabla ya kuanguka na kuchomeka.
Mkurugenzi mkuu wa Mamlaka ya usafiri wa anga nchini KCAA, Emile Arao, alisema ndege hiyo ndogo yenye nambari ya usajili 5Y-CCA ilikuwa na abiria 12 wenye asili ya Ugerumani ambao walikuwa wameabiri ndege hiyo.
Arao alisema tayari maafisa wa usafari wa angani wameanzisha uchunguzi ili kubaini kiini cha ajali hiyo kwani hata mabaki ya ndege hiyo yalichomeka.


Taarifa ya Mamlaka ya usafiri wa anga nchini KCAA kuhusu kuanguka kwa ndege ya 5Y-CCA
Ajali hiyo ya ndege imetokea miezi kadhaa baada ya ndege ndogo ya Wanajeshi kuanguka katika kaunti hiyo ya Kwale kutokana na changamoto za kimitambo.
Hii sio mara ya kwanza mikasa ya ndege kuanguka kushuhudiwa katika ukanda wa Pwani ambapo ndege yengine ndogo ilikuwa katika mafunzo ya marubani ilikumbwa na hitilafu za kimitambo na kuanguka katika eneo la Kwa Chocha mjini Malindi.
Ajali hiyo ya Malindi ilisababisha vifo vya watu wawili ingawa changamoto kubwa ni kwamba hakujakuwa na taarifa zozote kuhusu ripoti ya kilichosababisha ajali hiyo na hata fidia kwa familia zilizopoteza wapendwa wao.
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

