News
Wito wa haki kupatikana watawala mazishi ya Albert Ojwang’
Ibada ya mazishi kwa ajili ya mwendazake mwanablogu na mwalimu Albert Ojwang’ aliyeuawa mikononi mwa polisi inafanyika katika shule ya msingi ya Nyawango kaunti ya Homa Bay, huku kukiwa na hali ya taharuki.
Katika hafla hiyo uwepo wa maafisa wa usalama haujashuhudiwa.
Kulingana na Odhiambo Ojiro, mmoja wa wanaharakati katika eneo hilo alisema vijana wamejitolea kumpumzisha Ojwang’ kwa heshima aliyostahili’ na ishara hiyo imeonyesha umoja walionao vijana hao.
Wakizungumza katika hafla hiyo, baadhi ya walimu katika shule ambayo Albert alikuwa akihudumu katika kaunti ya Taita Taveta, wakiongozwa na Ismael Omoke Kongo walishinikiza naibu inspekta jenerali wa Eliud Lagat na wengine waliohusika na mauaji hayo kukamatwa na kufunguliwa mashtaka mahakamani.
Walisema kesi ya mauaji ya dhidi ya Albert inafaa kuchukuliwa kwa uzito na kuharakishwa mahakamani ili haki kwa familia na jamii ipatikane.
“Tunataka hii kesi kuharakishwa na wote waliohusishwa iwe kupitia kutoa maagizo hadi utekelezaji kushtakiwa”, walisema walimu hao
Wanablogu mbali mbali waliofika katika hafla hiyo waliunga mkono kauli ya walimu hao huku wakishikiniza mamlaka ya kutathmini utendakazi wa polisi IPOA na idara ya upelelezi wa makosa ya jinai DCI kuwajibika.
“Yale ambayo mnatenda Mungu anaona, ipo siku sauti zetu zitasikika, mimi naambia IPOA na DCI mnatatiza haki kwa Albert na nataka mmkamate mshtakiwa, na tunaambia serikali huwezi kutuua na utuongoze”, walisema wanablogu.
Ojwang’ alichukuliwa nyumbani kwao kaunti ya Homabay na maafisa wa usalama na kusafirishwa hadi kituo cha polisi cha Central jijini Nairobi ambapo alitangazwa kufariki baadaye.
Wakati huo polisi walitoa taarifa na kudai Albert alifariki baada ya kujigonga kwenye ukuta wa chumba cha seli alimokuwa anazuiliwa kituoni Central.
Mauaji ya Albert yalizua hasira miongoni mwa wakenya hasa vijana wa kizazi cha Gen Z, ambao wamekuwa wakiendeleza misururu ya maandamano nchini.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

