News
IEBC imepongeza zoezi la usajili wa wapiga kura wapya
Naibu Mwenyekiti wa tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC Fahima Araphat amesema zoezi la usajili wa wapiga kura wapya linaendelea vyema licha ya changamoto mbalimbali.
Akizungumza katika ukumbi wa Kibaoni mjini Kilifi kaunti ya Kilifi kwenye hafla ya ushirikishaji wadau katika kutoa maoni kuhusu namna zoezi hilo linavyotekelezwa kaunti ya Kilifi, Araphat alisema kufikia Aprili 15 walikuwa wamesajili watu milioni 1.3.
Araphat pia alisema wakenya wanaendelea kujitokeza katika zoezi hilo na mikakati ifaayo imewekwa kuhakikisha wananchi wote wanasajiliwa kuwa wapiga kura ili washiriki uchaguzi mkuu ujao wa 2027 na kujitenga na madai kuwa IEBC inaegemei mrengo flani wa kisiasa.
‘’Sisi kama tume tutahakikisha kuna uwazi katika usajili huu na hata wakati wa kuandaliwa kwa uchaguzi mkuu na tunaomba Wakenya wajitokeze kwa wingi kusajiliwa kuwa wapiga kura kabla ya kukamilika Aprili 28’’ Alisema Araphat
Wakati huohuo, Araphat akigusia suala la uratibu wa mipaka, alisema tume ya IEBC haiwezi kufanya uratibu huo kwa sasa ila mikakati inawekwa kuhakikisha unatekelezwa.
Naye meneja wa uchaguzi wa kaunti ya Kilifi Juma Musa Juma alitoa wito kwa wadau mbalimbali kushirikiana na IEBC ili fanikisha zoezi hilo la usajili wa wapiga kura wapya akitaja eneo bunge la Magarini kama ambalo linaongoza kwa usajili huo.
‘’ Tunahitaji ushirikiano wa kila mtu na idara ili zoezi ili litekelezwe kama lilivyoratibiwa’’ Alisema Musa
Kwa upande wake mwakilishi wa wadi ya Kibarani Moses Furaha Kea, alitoa wito kwa IEBC kuhakikisha idara inayohusika na usajili wa vitambulisho inaharakisha katika utoaji ili wananchi waweze kujisajili kuwa wapiga kura.
Nao wananchi waliohudhuria hafla hiyo waliitaka IEBC kufika mashinani ili kusajili idadi kubwa ya wapiga kura na kuwahimiza wananchi kujitokeza kwa wingi kusajiliwa huku kamanda wa polisi eneo bunge la Kilifi Kaskazini Stanley Tunui na naibu kamishna wa Kilifi Kaskazini Samuel Mutisya wakisema idara ya usalama iko imara katika kuhakikisha usalama unaimarishwa vilivyo.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Jubilee yaunga mkono maandamano ya kupinga bei ya mafuta
Kufuatia sakata ya uagizaji wa mafuta ghushi nchini, sasa Muungano wa upinzani umetishia kufanya maandamano kuanzia wiki ijayo.
Mwenyekiti wa kitaifa wa Chama cha Jubilee Vincent Kemosi, alisema maandamano hayo yanalenga kushinikiza kupunguzwa kwa bei ya mafuta nchini, akimshtumu Rais William Ruto kwa kuchangia mahangaiko wakenya.
Katika kikao na Wanahabari mjini Kilifi kaunti ya Kilifi baada ya kufanya kifanya kikao na viongozi wa chama hicho kanda ya Pwani, Kemosi aliikosoa serikali, akisema wakenya wamechoka kudanganywa na serikali iliyofeli kutekeleza ahadi zake.
“Serikali imeonyesha kushindwa kutatua suala la mafuta na imeonyesha wazi kwamba imefeli, huezi badilisha ushuru wa mafuta baada ya wananchi kulalamika mbona hakufanya hivyo tangu mwanzo, wakenya wamechoka”, alisema Kemosi.
Kemosi, amepinga mpango wa kugawa maeneo kisiasa yaani Zoning, akisema Viongozi wa Chama cha Jubilee watazingatia haki na usawa pamoja na kuandaa uchaguzi wa mashinani wa viongozi wa chama hicho, kauli iliyoungwa mkono na Mwenyekiti wa chama hicho kaunti ya Kilifi Anthony Kingi.
“Katika ya Kenya haijasema mambo ya Zoning, kila mtu ana haki ya kupigania wadhfa anataka, na sisi kama Chama cha Jubilee hatuingi mkono mambo ya zoning, tutahakikisha uchaguzi unafanyika mashinani kwa haki na uwazi”aliongeza Kemosi.

Viongozi wa Chama cha Jubilee wakiongozwa na Mwenyekiti wa kitaifa wa Chama hicho wafanya mkutano wa kuimarisha chama mashinani, Kilifi
Viongozi hao pia waliwarai wananchi kutathmini viongozi wao na kujiunga na vyama vinavyozingatia haki na usawa, wakisisitiza kuunga mkono upinzani.
Katika swala la raslimali, viongozi hao wameshtumu kutengwa kwa raslimali za Pwani hasa zao la mzani na mkorosho, wakisema wakati umefika kwa mpwani kutambulika na raslimali zake kuthaminiwa.
“Zao la Mnazi na Mkorosho ambayo ndio raslimali ya mpwani imetengwa tangu taifa ipate uhuru ndio sisi tunasema ni lazima raslimali ya mpwani pia nayo itambulike kikamilifu”, alisema Garama.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi.
News
Meli yenye bendera ya Kenya yazuiliwa Tanzania
Mamlaka ya usafiri wa majini nchini (KMA), imethibitisha kupokea taarifa kuhusu kuzuiliwa kwa meli yenye bendera ya Kenya katika nchi ya Tanzania.
Kupitia taarifa kwa vyombo vya habari, KMA imesema meli hiyo inayojulikana kama MV SEA MFALME kwa sasa inashikiliwa nchini humo.
Maafisa wa Mamlaka hiyo, wale wa ujasusi, na wanajeshi wa majini wameanzisha uchunguzi kubaini sababu za tukio hilo, na kama meli hiyo ilikuwa imebega shehena gani ndiposa ikazuiliwa.
Mamlaka hiyo imeeleza kuwa inashirikiana kwa karibu na mashirika ya kiserikali pamoja na wadau katika nchi zote mbili ili kubaini kilichosababisha kuzuiliwa kwa meli hiyo na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa.
Mamlaka hiyo ilielezwa kwamba tayari imeijulisha Wizara ya masuala ya kigeni nchini inayoongozwa na Waziri Musalia Mudavadi ili kusaidia katika masuala ya kidiplomasia kwani hatua hiyo huenda ikachangia sintofahamu za kimataifa.
KMA imewahakikishia wadau wa sekta hiyo na wamiliki wa meli hiyo kuwa suala hilo linashughulikiwa kwa kufuata taratibu za kisheria na ushirikiano wa kimataifa, na kwamba taarifa zaidi zitatolewa kadri uchunguzi unavyoendelea.
“Tunashirikiana na wadau mbalimbali kwa kuzingatia sheria za kimataifa na ushirikiano wa kidiplomasia kuhusu suala hilo na kwamba hatua za kisheria zitachukuliwa”, alieleza afisa mmoja wa Mamlaka hiyo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

