News
Mahakama ya Kilifi yawatupa gerezani washtakiwa zaidi ya 10
Mahakama ya Kilifi imetoa hukumu kwa washtakiwa zaidi ya 10 waliowasilishwa Mahakamani wakikabiliwa na mashtaka mbalimbali ikiwemo kesi za unajisi na makosa ya jinai.
Katika vikao vya Mahakama siku ya Jumatano tarehe 3 June 2026, Hakimu Ivy Wasike ametoa hukumu hizo kwa watuhumiwa hao huku wengine wakifungwa kwa zaidi ya miaka 30 gerezani.
Simon Ngala, Aliwali Ali Mwalimu, Christopher Buru, miongoni mwa wengine zaidi ya 10 walifikishwa katika Mahakama ya Kilifi na kuhukumiwa kufuatia mashtaka mbalimbali yanayowakabili ikiwemo mashtaka ya unajisi na makosa ya jinai.
Hakimu wa Mahakama ya Kilifi Ivy Wasike, alimhukumu kifungo cha miaka 30 gerezani Simon Ngala baada ya kupatikana na hatia ya kumnajisi mtoto wa miaka 13 kisha akamtorosha kwao kwa kipindi cha mwezi mzima.
Mwengine ni Aliwali Ali Mwalimu, aliyehukumiwa kifungo cha miaka 25 kufuatia mashtaka ya kumpachika ujauzito mtoto wa miaka 13 licha ya kuomba msamaha Mahakamani.
Wakati wa kutoa hukumu hizo, Hakimu Wasike alisikitishwa na kukithiri kwa visa vya watoto kupotea na kisha kunajisiwa katika kaunti ya Kilifi.
Kiongozi wa mashtaka katika Mahakama hiyo Nancy Njeru alipinga vikali ombi lililowasilishwa Mahakama la kutaka washtakiwa wasamehewe, kwanin wengine walidai kwamba walishirika makosa hayo bila kukusudia, akisema hukumu hizo zitakuwa funzo kwa watu wenye hulka hizo katika jamii.
Mbali na hukumu za kesi za unajisi, Christopher Buru alihukumiwa kifungo cha miaka miwili gerezani akikabiliwa na mashtaka ya wizi baada ya kupatikana na hatia ya kutumia pesa za mlalamishi Saumu Nyevu aliyekuwa akimtumia pesa alipokuwa akifanya kazi katika milki za kiarabu, kosa lililomchukiza zaidi Hakimu Wasike.
Taarifa ya Teclar Yeri
News
Mbunge wa Nyali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila
Mbunge wa Nyali kaunti ya Mombasa Mohamed Ali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila kwenye kaunti hiyo, akisema anafanya siasa zake bila kujali dini, kabila au hata eneo.
Akizungumza huko Nyali, Ali alisema kuna baadhi ya viongozi katika kaunti ya Mombasa, ambao wamekuwa wakiendekeza propaganda za kumhusisha na siasa za migawanyiko ili kumharibia jina taifa linapojiandaa kwa uchaguzi mkuu ujao wa 2027.
Ali ambaye alitangaza kuwania wadhifa wa ugavana kaunti ya Mombasa, aliwataka viongozi kufanya siasa zao kwa kunadi sera zao kwa wakaazi na maendeleo ambayo watatekeleza na sio kutumia suala la ukabila kuwachafulia wengine jina.
“2017 hakuna mtu aliniita mkabila, 2022 hakuna mtu aliniita mkabila, 2027 wanasema Mohamed Ali ni mkabila.Mimi Mohamed Ali, mimi nauliza nikisimama hapa juu ya gari, niseme kabila zote za Kenya wanaweza pewa nafasi ya ugavana ni kuna makosa?,basi sasa wanazunguka wakisema Mohamed ni mkabila kwasababu ameanza kufungua watu macho’’ alisema Ali.
Aidha, Ali alisema ataendelea kuzuru maeneo mbalimbali ya kauti ya Mombasa kunadi sera zake na kuwataka wakaazi wa kaunti hiyo kuwachagua viongozi wanaofaa ambao wataimarisha kaunti hiyo kimaendeleo.
‘’Mimi nimewaambia nitatembea hii Mombasa kwa uwezo wake mwenyezi mungu kutetea wananchi wa Mombasa’’ aliongeza Ali
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Wakimbizi nusu milioni wakabiliwa na baa la njaa, Dadaab
Ripoti iliyotolewa hivi karibu na Shirika la Chakula duniani WFP ilionyesha kwamba zaidi ya wakimbizi nusu milioni wanaoishi katika kambi za wakimbizi za Kakuma na Dadaab zilizoko nchini Kenya, wako katika hatari ya kuangamia kutokana na baa la njaa.
Kambi hizi ambazo zinahifadhi wakimbizi wengi zaidi kutoka nchini Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Somalia, ziko hatari iwapo zitakosa misaada ya chakula.
Kufuatia hali hiyo ambayo pia imechangiwa na mashirika ya kimataifa kusitisha ufadhili, sasa hali huenda ikawa tofauti baada ya taifa la Korea kwa ushirikiano na Kenya kutoa ufadhili wa shehena ya nafaka ya zaidi ya tani elfu 10 ambayo inakadiriwa kuwa kima cha shilingi milioni 1.2.
Katibu katika Idara ya uhamiaji nchini Belio Kipsang, aliyepokea msaada huo wa Chakula mjini Mombasa na kuhifadhiwa katika maghala ya Shirika la WFP, ameonya kwamba iwapo Kenya itakosa kupokea msaada kutoka kwa washirika na wafadhili wengine, basi italazimika kuchukua maamuzi magumu, ikiwemo kuwaondoa baadhi ya wakimbizi.
“Nyuma ya kila takwimu kuna familia ambazo ustahimilivu wao unaendelea kujaribiwa kila siku: akina mama wanaokosa kula ili watoto wao wapate chakula, watu walio katika mazingira hatarishi wakiruka milo, na vijana wanaokabiliwa na mustakabali usio na uhakika. Hizi si takwimu za kufikirika. Zinawakilisha watu halisi ambao heshima yao, afya yao na matarajio yao ya maisha yanategemea maamuzi tunayofanya kwa pamoja,” alisema.
Wakati wa hafla hiyo ya kupokea msaada huo wa chakula kwa wakimbizi wa Kakuma na Dadaab, Mkurugenzi wa Shirika la WFP nchini Kenya Betty Ka, alisema shehena ya nafaka itasaidia kuwahudumia takribani wakimbizi nusu milioni katika miezi ijayo.
“Usafirishaji huu unaonyesha umuhimu wa ushirikiano imara katika mnyororo wa ugavi wa misaada ya kibinadamu, ambapo ushirikiano huu kati ya Kenya, Mamlaka ya bandari Kenya (KPA), Shirika la viwango la Kenya(KEBS) na mpango wa Chakula Duniani (WFP) kwa kuhakikisha kwamba chakula cha msaada kinafanikishwa”,alisema Betty.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

