News
Washukiwa 5 wa uhalifu wanazuiliwa na polisi Likoni
Maafisa wa polisi katika eneo bunge la Likoni kaunti ya Mombasa wanawazuiliwa washukiwa 5 wa uhalifu waliokamatwa katika oparesheni iliyofanyika maeneo ya Duduz na Bufallo siku ya Jumatatu tarehe mosi Juni 2026.
Washukiwa waliokamatwa ni Brian Musa mwenye umri wa miaka 24, Abubakar Mahasi wa umri wa miaka 20, Juma Kassim mwenye umri wa miaka 16, Omar Gobeko maarufu Mboga mwenye umri wa miaka 19 na Jackson Mwambu mwenye umri wa miaka 26.
Msako huo uliongozwa na mkuu wa kituo cha polisi cha Shelly Beach pamoja na kikosi cha maafisa wa polisi.
Maafisa wa Polisi wamesema mshukiwa Brian Musa anakabiliwa na tuhuma za maandalizi ya kutenda kosa la jinai, huku Ababakar Mahasi, Juma Kassim na Omar Gobeko wakihusishwa na tuhuma za wizi wa mabavu.
Mshukiwa mwengine Jackson Mwambu anahusishwa na tuhuma za kupatikana na mali ya serikali kinyume cha sheria.
Katika oparesheni hiyo, maafisa wa polisi walifanikiwa kupata vielelezo mbali mbali ikiwemo panga tatu pamoja na koti la jeshi la KDF.
Taarifa ya Joseph Jira
News
DCI waomba muda zaidi dhidi ya kesi ya Keziah
Mahakama ya Kilifi imeagiza kuendelea kuzuiliwa kwa siku 6 zaidi Alice Auma Omondi anayetuhumiwa kuhusika kwenye kesi ya mauaji ya mtoto Keziah aliyekuwa na umri wa miaka 7.
Hakimu wa Mahakama hiyo Ivy Wasike ametoa agizo hilo baada ya afisa anayechunguza kesi hiyo Evans Baraza kuiambia Mahakama kwamba bado hawajakamilisha uchunguzi wao.
Alice Auma Omondi anayedaiwa kuwa Mamake mshukiwa mkuu wa mauaji hayo Dennis Otieno Odour kwa jina maarufu Dennis Mkikuu alikamatwa kama mshukiwa wa kwanza na kufikishwa Mahakamani tarehe 6 mwezi Mei 2026 ambapo aliagizwa kuzuiliwa kwa wiki tatu ili ashirikiane na maafisa wa polisi kumtafuta mshukiwa mkuu.
Hata hivyo wiki moja baadaye mshukiwa mkuu Dennis alikamatwa na kufikishwa katika Mahakama ya Shanzu ambapo bado anazuiliwa kufuatia kesi ya mauaji dhidi yake.
Maafisa wa DCI wanamshuku Alice kwamba anahusika kwenye kesi hiyo kwa kuharibu ushahidi huku maafisa hao wakipendekeza kwamba Alice pia anafaa kufunguliwa mashtaka baada ya uchunguzi kamili.
Kesi hiyo itatajwa tarehe 8 mwezi huu wa Juni.
Taarifa ya Teclar Yeri
News
Polisi waonya wananchi dhidi ya mauaji ya wazee Kwale
Idara ya usalama kaunti ya Kwale imewaonya wananchi dhidi ya kuchukua sheria mikono na kusababisha maafa katika jamii kwa kisingizio cha kuwaua wazee kwa tuhma za uchawi.
Kamishna wa kaunti hiyo David Rotich alisema maafisa wa usalama wameanzisha msako mkali dhidi ya wale waliohusika katika matukio matano ya mauaji ya wazee.
Akizungumza katika bustani ya Baraza mjini Kwale, Rotich alisema mauaji dhidi ya wazee yameripotiwa kuchipuka upya na kwamba hivi karibuni katika eneo la Lungalunga na Kinango kumeripotiwa visa vitano vya mauaji ya wazee.
“Nimetoa amri kwa kamati ya usalama eneo la Lungalunga na Kinango kuhakikisha wale wanaohusika wanakamatwa na kufikishwa Mahakamani, hatuwezi ruhusu visa hivyo kuendelea na wazee ni watu muhimu katika jamii’, alisema Rotich.
Kwa upande wake Naibu Gavana wa Kwale Chimera Kombo amepongeza ushirikiano unaoendelea kati ya serikali kuu na kaunti ya Kwale, akisema umechangia wakaazi wa kaunti hiyo kushuhudia maendelea, akitoa mfano wa barabara ya Kwale-Kinango.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

