News
Mpango wa uagizaji mafuta wa G to G waingia dosari
Serikali imeendelea kujitetea kuhusu mpango wa uagizaji wa mafuta wa serikali kwa serikali maarufu kama G to G, huku viongozi wa kisiasa wakitoa mitazamo kinzani kuhusu utekelezaji wake.
Serikali kupitia Mamlaka ya kudhibiti bei za mafuta nchini EPPRA, imetangaza ongezeko la bei mpya za mafuta kwa shilingi 28 kwa lita moja ya mafuta ya petrol huku diseli ikiongezeka kwa shilingi 40 kwa lita.
Hatua hii imezua mjadala mkali kuhusu athari za mfumuko wa bei nchini.
Viongozi wa upinzani wakiongozwa na Kinara wa Chama cha DCP, Rigathi Gachagua, na Kinara wa Chama cha Wiper Kalonzo Musyoka wamekosoa vikali serikali kufutia ongezeko la bei ya mafuta wakisema mpango wa G to G ilikuwa ni njama ya kumfaidi Rais William Ruto, wakifichua kwamba takriban shilingi tano kwa kila lita ya mafuta itakayouzwa nchini itakuwa inamfaidi Rais Ruto.
Viongozi hao pia, walimtaka Waziri wa Kawi na Petroli nchini Opiyo Wandayi, pamoja na Waziri wa Biashara na Uwekezaji wa viwanda nchini Lee Kinyanjui, kujiuzulu.
Kwa upande wake mbunge wa Kiharu, Ndindi Nyoro pia ameukosoa mpango huo akidai kwamba ni njama ya baadhi ya viongozi wakuu serikalini kujinufaisha binafsi.
Nyoro aliema mpango huo ni njia ya kuwahadaa wakenya ilhali mzigo mkubwa unaishia kwa walipa ushuru.
Aliongeza kuwa mpango huo unanufaisha baadhi ya kampuni za mafuta nchini zinazodaiwa kumilikiwa na viongozi wa juu serikalini huku akitoa baadhi ya mapendekezo kwa serikali pamoja na wadau wa sekta ya kawi ambayo kulingana naye, yanaweza kushusha bei ya mafuta kwa takriban shilingi 27.
Hata hivyo, Rais William Ruto ametetea mpango huo akisema serikali imetumia takriban shilingi bilioni 6.5 kutoa ruzuku ya mafuta ili kupunguza mzigo kwa wananchi hasa ushuru wa VAT kwa asilimia 8.
Kwa upande wake, Waziri wa Kawi na Petroli nchini Opiyo Wandayi alisema serikali imejizatiti kukabiliana na wanaojihusisha na uagizaji wa mafuta ghushi humu nchini.
Hata hivyo, kumeshuhudiwa tofauti katika takwimu za fedha zilizotolewa kuhusu mpango huo, Rais akitaja bilioni 6.5 ilhali Waziri Wandayi akisema serikali iliwekeza takriban bilioni 6.2.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
IEBC: Vijana wanaitisha pesa kusajiliwa kuwa wapiga kura
Wakenya wanaojitokeza kujisajili kama wapiga kura katika zoezi endelevu lililoidhinishwa na Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC, inatia matumaini ya Tume hiyo kufikia malengo yake ya kusajili wa idadi ya watu milioni 6.2 kote nchini.
Katika kaunti ya Kilifi kwenye eneo bunge la Kilifi Kazkazini ambapo zoezi hilo linaendelea, Maafisa wa Tume hiyo wamedai kupitia changamoto wakati wa usajali wa wapiga kura.
Maafisa hao wanasema kati ya changamoto hizo ni pamoja na kuitishwa pesa na vijana ndipo wawasajili kuwa wapiga kura, wakisema changamoto hiyo inarudisha nyuma juhudi zilizoidhinisha na Tume ya IEBC.
Afisa anayesimamia Tume ya IEBC katika eneo bunge la Kilifi Kazkazini John Mwawasi alisema licha ya changamoto hizo, kufikia sasa maafisa wa tume hiyo wanaozuru nyanjani wamefanikiwa kusajili wapiga kura wapya kwa asilimia 50.
News
Jackson Chiwai ahukumiwa kifungo cha miaka 15 gerezani
Mahakama ya Kilifi imemhukumu kifungo cha miaka 15 gerezani Jackson Chiwai baada ya Mahakama kumpata na hatia ya kumnajisi mtoto mdogo wa umri wa miaka 5.
Hukumu hiyo imetolewa na Hakimu wa Mahakama hiyo Charles Obulutsa baada ya ushahidi kamili kuwasilishwa Mahakamani.
Hakimu Obulutsa alisema kwamba hukumu hiyo imezingatia ushahidi wote uliyowasilishwa Mahakamani kiwemo ripoti ya daktari kuhusu uchunguzi wa unajisi dhidi ya mtoto huyo.
Kabla ya hukumu hiyo kutolewa, upande wa mashtaka ukiongozwa na Kiongozi wa mashtaka ya umma katika Mahakama hiyo Ridhwan Mohammed ulieleza Mahakama kwamba mnamo tarehe 11 mwezi Mei mwaka 2024 mwendo wa saa moja jioni Jackson alimnajisi mtoto wa miaka 5 ambaye ni binamu yake.
Japo ushahidi wa mlalamishi na mashahidi wengine ambao ni watoto wenzake uliashiria kitendo hicho cha unajisi kuwa kweli baada ya watoto hao kueleza Mahakama kwamba walikuwa wakiangalia runinga chumbani wakati mama yao akiwa jikoni akipika, ambapo Jackson ambaye ni binamu yao aliingia chumbani humo na kumchukua mtoto huyo na kutoka naye nje ambapo alitekeleza kitendo hicho.
Kulingana na ushahidi wa daktari, uchunguzi na vipimo kwa mtoto huyo ilionyesha kwamba mtoto hakuwa amenajisiwa bali kulikuwa na jaribio la dhulma ya kingono kutokana na mikwaruzo kwenye uke wa mtoto huyo.
Uchunguzi wa daktari ulichangia pakubwa kwenye hukumu hiyo ambayo Hakimu Obulusta alieleza kwamba Jackson angehukumiwa kifungo cha maisha kulingana na sheria na uzito wa kesi hiyo.
Mshukiwa alihukumiwa kwa kosa mbadala la kujaribu kumnajisi mtoto huyo na kupata kifungo hicho cha miaka 15.
Mahakama hata hivyo imempa mshtakiwa siku 14 za kukata rufaa iwapo hajaridhishwa na uamuzi wa Mahakama.
Taarifa ya Teclar Yeri.

