News
Msako wa kukabiliana na MAWOZA waidhinishwa Kilifi
Idara ya usalama kaunti ya Kilifi inapoendeleza mikakati ya kukabiliana na magenge ya kihalifu maarufu ‘Mawoza’, visa vya watu kuvamiwa vingali vinaendelea kushuhudiwa mjini Malindi kaunti ya Kilifi.
Kisa cha hivi punde kikiwa cha mwanaume mmoja ambaye alivamiwa na kukatwa mapanga na watu wanaoaminika kuwa “mawoza” vijana wanaoshiriki uhalifu eneo la Shela, Malindi kaunti ya Kilifi.
Taarifa zinasema kuwa mwanaume huyo alikuwa akielekea kuswaali alfajiri kabla ya kupatana na wahalifu hao, kisa ambacho kimethibitishwa na naibu Chifu eneo hilo, Nicodemus Mwayele, alipozungumza na COCO FM kwa njia ya simu kuhusu tukio hilo.

Wakaazi wanaitaka idara ya usalama kukabiliana kikamilifu na kundi la wahalifu la Mawoza kaunti ya Kilifi
Haya yanajiri, msako ukiendelezwa na kikosi maalumu cha usalama katika kaunti ya Kilifi kukabiliana na ‘MAWOZA’ huku baadhi ya wakaazi wakiibua hisia mbalimbali wakisema huenda msako huo ukasaidia kwa asilimia kubwa kuwakamata wanaojihusisha na visa hivyo ili wakabiliwe kisheria.
Wengine wamesema huenda juhudi hizo zikakosa kuzaa matunda wakidai licha ya wanaojihisha na visa hivyo kakamatwa huwa hawafikishwi Mahakamani kufunguliwa mashtaka.
Msako huo unajiri siku chache baada ya gavana wa kaunti ya Kilifi Gedion Maitha Munga’aro kuandaa kikao cha faragha na kamanda wa polisi ukanda wa pwani Ali Nuno, naibu kamishna wa eneo bunge la Kilifi Kaskazini Samuel Muinde Mutisya, kamanda wa polisi kaunti ya Kilifi Reginald Omaria, Mbunge wa Kilifi Kaskazini Owen Baya, Mbunge wa Malindi Amina Mnyazi na wakuu wengine wa usalama kaunti ya Kilifi.
Taarifa ya Janet Shume
News
Mbunge wa Nyali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila
Mbunge wa Nyali kaunti ya Mombasa Mohamed Ali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila kwenye kaunti hiyo, akisema anafanya siasa zake bila kujali dini, kabila au hata eneo.
Akizungumza huko Nyali, Ali alisema kuna baadhi ya viongozi katika kaunti ya Mombasa, ambao wamekuwa wakiendekeza propaganda za kumhusisha na siasa za migawanyiko ili kumharibia jina taifa linapojiandaa kwa uchaguzi mkuu ujao wa 2027.
Ali ambaye alitangaza kuwania wadhifa wa ugavana kaunti ya Mombasa, aliwataka viongozi kufanya siasa zao kwa kunadi sera zao kwa wakaazi na maendeleo ambayo watatekeleza na sio kutumia suala la ukabila kuwachafulia wengine jina.
“2017 hakuna mtu aliniita mkabila, 2022 hakuna mtu aliniita mkabila, 2027 wanasema Mohamed Ali ni mkabila.Mimi Mohamed Ali, mimi nauliza nikisimama hapa juu ya gari, niseme kabila zote za Kenya wanaweza pewa nafasi ya ugavana ni kuna makosa?,basi sasa wanazunguka wakisema Mohamed ni mkabila kwasababu ameanza kufungua watu macho’’ alisema Ali.
Aidha, Ali alisema ataendelea kuzuru maeneo mbalimbali ya kauti ya Mombasa kunadi sera zake na kuwataka wakaazi wa kaunti hiyo kuwachagua viongozi wanaofaa ambao wataimarisha kaunti hiyo kimaendeleo.
‘’Mimi nimewaambia nitatembea hii Mombasa kwa uwezo wake mwenyezi mungu kutetea wananchi wa Mombasa’’ aliongeza Ali
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Wakimbizi nusu milioni wakabiliwa na baa la njaa, Dadaab
Ripoti iliyotolewa hivi karibu na Shirika la Chakula duniani WFP ilionyesha kwamba zaidi ya wakimbizi nusu milioni wanaoishi katika kambi za wakimbizi za Kakuma na Dadaab zilizoko nchini Kenya, wako katika hatari ya kuangamia kutokana na baa la njaa.
Kambi hizi ambazo zinahifadhi wakimbizi wengi zaidi kutoka nchini Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Somalia, ziko hatari iwapo zitakosa misaada ya chakula.
Kufuatia hali hiyo ambayo pia imechangiwa na mashirika ya kimataifa kusitisha ufadhili, sasa hali huenda ikawa tofauti baada ya taifa la Korea kwa ushirikiano na Kenya kutoa ufadhili wa shehena ya nafaka ya zaidi ya tani elfu 10 ambayo inakadiriwa kuwa kima cha shilingi milioni 1.2.
Katibu katika Idara ya uhamiaji nchini Belio Kipsang, aliyepokea msaada huo wa Chakula mjini Mombasa na kuhifadhiwa katika maghala ya Shirika la WFP, ameonya kwamba iwapo Kenya itakosa kupokea msaada kutoka kwa washirika na wafadhili wengine, basi italazimika kuchukua maamuzi magumu, ikiwemo kuwaondoa baadhi ya wakimbizi.
“Nyuma ya kila takwimu kuna familia ambazo ustahimilivu wao unaendelea kujaribiwa kila siku: akina mama wanaokosa kula ili watoto wao wapate chakula, watu walio katika mazingira hatarishi wakiruka milo, na vijana wanaokabiliwa na mustakabali usio na uhakika. Hizi si takwimu za kufikirika. Zinawakilisha watu halisi ambao heshima yao, afya yao na matarajio yao ya maisha yanategemea maamuzi tunayofanya kwa pamoja,” alisema.
Wakati wa hafla hiyo ya kupokea msaada huo wa chakula kwa wakimbizi wa Kakuma na Dadaab, Mkurugenzi wa Shirika la WFP nchini Kenya Betty Ka, alisema shehena ya nafaka itasaidia kuwahudumia takribani wakimbizi nusu milioni katika miezi ijayo.
“Usafirishaji huu unaonyesha umuhimu wa ushirikiano imara katika mnyororo wa ugavi wa misaada ya kibinadamu, ambapo ushirikiano huu kati ya Kenya, Mamlaka ya bandari Kenya (KPA), Shirika la viwango la Kenya(KEBS) na mpango wa Chakula Duniani (WFP) kwa kuhakikisha kwamba chakula cha msaada kinafanikishwa”,alisema Betty.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

