News
Panda shuka za kiuongozi katika serikali za ugatuzi
Huku Kongamano la Ugatuzi awamu ya 12 likiendelea kaunti ya Homa Bay, bado Wakenya wanaendelea kutathmini iwapo malengo ya ugatuzi yanatimizwa.
Yapo maswali mengi tu kuhusu ufanisi wa kimaendeleo na utenda kazi wa serikali za kaunti ambazo hadi sasa nyingi zao zinazidi kulaumiwa kwa kuendeleza ufisadi, usimamizi mbaya wa rasilimali, na utoaji wa huduma duni, suala ambalo limeendelea kuwamulika magavana na maafisa wengine wa serikali za kaunti.
Tangu Ugatuzi uanzishwe baada ya katiba mpya ya mwaka 2010, Bunge la seneti limetenga takribani shilingi trillioni 4 kwa serikali za ugatuzi kupitia mfumo wa ugavi wa rasilimali za serikali kwa huduma za kaunti, ingawa bado kuna maswali mengi kuliko majibu kuhusu malengo yaliyokusudiwa sheria hii ya ugatuzi.
Uongozi wa serikali hizi bado upo kwenye mizani na mitihani mingi tu, ikiwa ni pamoja na ahadi nyingi zinazotolewa na viongozi wa serikali hizi za kaunti ambazo hazitimizwi kutokana na kile wananchi wanadai ni ukiritimba unaotokana na uongozi mbaya, ufisadi na upendeleo katika utoaji wa huduma na kandarasi.
Suala la utoaji wa kandarasi limekuwa donda sugu katika serikali nyingi za kaunti, huku zikiendelea kukabiliwa na malimbikizi ya madeni.
Miongoni mwa sekta zinazotajwa kuathirika zaidi na usimamizi mbaya au ufujaji wa pesa za umma ni sekta ya afya ambayo. Hospitali nyingi hazina dawa huku huduma za afya zikiendelea kudorora kuanzia ngazi za zahanati hadi hospitali kubwa za kaunti.
Serikali za kaunti pia zinashtumiwa kwa kuendelea na uratibu wa miradi hewa katika bajeti zao, na kupelekea kupotea kwa mabilioni ya pesa za uma.
Japo Ugatuzi ulilenga kuboresha maisha ya Wananchi katika ngazi za chini, bado umaskini umekithiri huku mizozo ya uongozi na utawala wa kibepari vikiendelea kushuhudiwa kati ya mabunge ya kaunti na ofisi za magavana.

Wanawake wakichota maji kutokana na manufaa ya ugatuzi {picha kwa hisani}
Matokeo ya mizozo hiyo mara nyingi yamekuwa kushuhudiwa kwa mapinduzi katika usimamizi wa ofisi za magavana kupitia hoja za kutokuwa na Imani nazo, au kutokuwa na Imani na usimamizi wa mabunge ya kaunti na Maspika wa mabunge hayo, hatma yake ikiwa ni kushinikizwa kutimuliwa kutoka ofisi zao.
Taarifa ya Eric Ponda
News
Rais Ruto atia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya uwekezaji wa mali
Rais William Ruto ametia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya kitaifa ya uwekezaji wa mali (Sovereign Wealth Fund), hatua inayotajwa kuwa muhimu katika juhudi za Kenya za kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kulinda utajiri wa taifa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa muda mrefu.
Utiaji huo wa saini ulifanyika katika Ikulu ya Nairobi na unaweka msingi wa kisheria wa kuanzishwa na kusimamiwa kwa mfuko wa taifa wa uwekezaji wa mali na kwamba unatarajiwa kuiwezesha nchi kuhifadhi rasilimali za umma zinazobaki baada ya matumizi ya kawaida, kufadhili uwekezaji wa kimkakati na kuimarisha uwezo wa uchumi kukabiliana na misukosuko ya kifedha siku zijazo.
Sheria hiyo mpya inaleta mfumo rasmi wa usimamizi wa utajiri wa taifa kwa kutenga akiba kwa ajili ya vizazi vijavyo, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili uwekezaji katika miundombinu ya kimkakati ili kuongeza uimara wa kifedha nchini pamoja na kuhimiza matumizi yenye uwajibikaji ya rasilimali za umma.
Mfuko huo utatumika kuwekeza mapato ya ziada yanayotokana na rasilimali za asili na mali nyingine za umma, kwa lengo la kuhakikisha manufaa yake yanawanufaisha wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
Aidha, mfuko huo unakusudia kupunguza athari za changamoto za kiuchumi kwa kutoa kinga ya kifedha wakati wa misukosuko ya uchumi.
Sheria hiyo ni sehemu ya ajenda pana ya serikali ya mageuzi ya uchumi inayolenga kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kuongeza uwazi na kuendeleza maendeleo endelevu.
Pia, sheria hiyo imeweka mfumo wa uongozi na usimamizi wa mfuko huo, ukiwemo utaratibu wa kuhakikisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi madhubuti katika uwekezaji na matumizi ya rasilimali za umma.
Maafisa wa serikali wameeleza kuwa Mfuko wa Taifa wa Uwekezaji wa Mali utakuwa na mchango mkubwa katika kufadhili miradi ya maendeleo yenye kipaumbele nchini huku ukihifadhi utajiri wa taifa kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
Kupitishwa kwa sheria hiyo kunaiweka Kenya miongoni mwa mataifa yanayoongezeka duniani ambayo yameanzisha mifuko ya taifa ya uwekezaji wa mali kwa lengo la kulinda mali za taifa, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili malengo ya maendeleo ya muda mrefu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
IEBC yakosolewa dhidi ya masharti mapya kwa wanasiasa
Kiongozi wa vijana katika Chama cha Wiper kaunti ya Kwale Nyawa Masai ameikosoa Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC kutokana na masharti mapya iliyotoa dhidi ya wanasaisa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Nyawa ameitaka Tume hiyo kuzingatia kanuni zake na taratibu za kuandaa uchaguzi na wala sio kila uchao kutoa masharti ambayo yanakinzana na majukumu ya Tume, akisema kuna taasisi zengine za umma zinafaa kuwajibika.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa katika eneo la Mwereni gatuzi dogo la Lungalunga kaunti ya Kwale, Nyawa aliesisitiza haja ya wanasiasa kupewa nafasi ya kuzungumza na wananchi sawa na kueleza sera zao bila ya vizuizi.
Kiongozi huyo wa vijana ambaye alitangaza nia yake ya kuwania kiti cha uwakilishi wadi ya Mwereni wakati wa uchaguzi ujao, amesema taifa la Kenya linazingatia demokrasia na kwamba kila taasisi inafaa kutekeleza majukumu yake.
“Katika uwaja wa siasa IEBC inakuzi moja tu kama msimamizi na kama msimamizi anaanza kutengeza sheria hapo ndipo anakosea, hii Kneya ni nchi ya demokrasia kwa hivyo IEBC isilete sheria nyingi na kufuatilia wanasiasa kuhusu pesa watatumia kwa kampeni, hiyo sio jukumu lake kuna taasisi inaitwa EACC”, alisema Nyawa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

