News
UDA yafanya awamu ya pili ya uchaguzi wa viongozi mashinani
Awamu ya pili ya zoezi la uchaguzi wa viongozi wa mashinani wa chama cha UDA imefanyika katika kaunti 18 kote nchini.
Zoezi hilo lilifanyika katika kaunti 6 za pwani pamoja na kaunti za Kisumu, Siaya, Migori, Kisii, Bungoma, Makueni, Machakos, Kitui, Isiolo, Marsabit na Turkana ili kuwachagua viongozi wa mashinani wa UDA.
Wagombea wa nyadhifa mbali mbali walijitokeza katika zoezi hilo ambalo lilivutia umati wa watu katika baadhi ya vituo.
Baadhi ya wagombea walieleza kuridhishwa na utaratibu wa zoezi hilo huku baadhi wakilalamikia changamoto za kimitambo katika baadhi ya vituo hali iliyowaacha baadhi ya wapiga kura nje.
Katika kituo cha shule ya msingi ya Kilifi mjini Kilifi, baadhi ya wagombea walilalamikia kuchezewa shere na wenzao, baada ya orodha ya majina kubatilishwa na kusababisha mchanganyiko miongoni mwa wafuasi wao.
Viongozi wakuu ndani ya chama cha UDA akiwemo mwenyekiti wa bodi ya barabara nchini Aisha Jumwa alipiga kura katika wadi ya Kakuyuni kuchagua viongozi hao wa mashinani.

Mgombea wadhfa wa useneta katika kaunti ya Kilifi kwenye uchaguzi mkuu wa 2027 Wakili George Kithi akizungumza na wakaazi.
Hata hivyo wakaazi wengi walisema zoezi hilo lilifanyika bila ya hamasa ya kutosha.
Wagombea wengi walieleza imani na zoezi hilo katika harakati za kuongoza chama cha UDA kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2027.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Polisi kutumia nguvu kukabiliana na wahalifu
Huenda maafisa wa polisi wakutumia nguvu kupita kiasi katika kukabiliana na wahalifu ama wale wanaolenga kuzua vurugu na fujo mashinani.
Idara ya usalama nchini imesisitiza kwamba itakabiliana kikamilifu na magenge ya kihalifu ambayo yanaendeleza uhalifu mashinani na kutatiza shughuli za kibiashara, uchumi na usalama wa taifa.
Idara hiyo ilisema tayari imebaini magenge ya kihalifu ambayo yanatatiza usalama wa wananchi, huku wazazi wakilaumiwa kwa kuwatetea watoto wao licha ya kufahamu kwa tabia hiyo inazidi kuhatarisha maisha ya jamii mashinani.
Idara hiyo, ililalamikia kukithiri kwa utovu wa usalama hasa kaunti za Kwale, Mombasa na Lamu katika ukanda wa Pwani, kutokana na vijana wengi kuzama katika uraibu wa Mihadarati na ukosefu wa kazi, hatua iliyopelekea baadhi ya vijana kujiunga na magenge ya mapanga.
Kauli hiyo ya idara ya usalama ilijiri siku moja tu baada ya Kamanda wa Polisi kanda ya Pwani Ali Nuno, kuagiza maafisa wa polisi kuwapiga risasi magenge ya kihalifu ya vipanga kwa kutatiza usalama.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Mswada wa marekebisho ya Katiba wa mwaka 2026 umewasilishwa bungeni
Mswada wa marekebisho ya Katiba wa mwaka 2026 na sheria za uchaguzi umewasilishwa katika bunge la Seneti.
Mswada huo unalenga kufanyia marekebisho kipengele cha Katiba cha 99 na 193 pamoja na sheria za uchaguzi sehemu ya 24 na 25 ili kuwepo na uwazi kwa magavana wanaolenga kuwania nyadhfa za uongozi baada ya kukamilisha mihula yao.
Mswada huo uliowasilishwa na Seneta wa Kirinyaga James Murango unalenga pia kuzuia magavana waliomaliza mihula yao ya uongozi kutowania nyadhfa za useneta, ubunge ama uwakilishi wadi, kwani inakuwa vingumu kuchunguzwa.
Kuwasilishwa kwa mswada huo bungeni kufuatia hali magavana kuwania wadhfa wa useneta baada ya kukamilisha mihula yao ya uongozi hali ambayo imeleta sintofahamu ya kiuongozi, ikiashiria tamaa za uongozi na njama ya kuhitilafiana na ufuatiliaji wa matumizi ya raslimali za umma.
Seneta Murango alisema katika utekelezaji wa majukumu yao, magavana hulazimika kuwajibika mbele ya mabunge ya kaunti na Seneti kuhusu matumizi ya kifedha na kiutawala.
Wakati huo huo alidokeza kwamba iwapo mswada huo utapishwa na kuwa sheria utasaidia kufutilia usimamizi wa raslimali za kaunti na matumizi ya fedha kwani utazuia magavana kuhitilafiana na uchunguzi.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

