News
Wahudumu wa Tuktuk Malindi washinikiza uhamisho wa Trafiki.
Wahudumu wa sekta ya Tuktuk mjini Malindi kaunti ya Kilifi wamelalamika kuhangaishwa na maafisa wa trafiki mjini humo licha ya kutimiza vigezo hitajika vya kuwaruhusu kuhudumu barabarani.
Mwenyekiti wa wahudumu hao kaunti ya Kilifi Abdhalla Mwangi alisema kuwa serikali inafaa kukifanyia mabadiliko kitengo hicho ili kutatua mzozo uliopo baina ya wahudumu hao na maafisa wa trafiki.
Mwangi alisistiza haja ya swala hilo kuangaziwa kwa kina kutokana na kile alichodai kuwa hali hiyo imeathiri pakubwa sekta hiyo kiuchumi.
“Hawa trafiki hawaturidishi kabisa, Malindi ulikuwa ni mji mzuri ambao unautulivu saa hii unaweza kubebwa na dereva, atazunguka kitambo afike mahali anaenda yaani hata wewe mwenyewe utamuonea huruma, hawa jamaa wamekuwa niusumbufu saa hii sio oparesheni”, alisema Mwangi.
.
Maafisa wa trafiki katika barabara za humu nchini(picha kwa hisani)
Mwangi aidha alibainisha kuwa licha ya kuwasilisha ombi la kutaka uhamisho wa maafisa wa trafiki waliohudumu kwa muda mrefu mjini humo, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa na serikali kufikia sasa
“Nilizungumza na serikali kuwaomba kwamba kuna maafisa wa trafiki hapa kwetu ambao hawana nidhamu za kikazi na wanagonganisha madereva na serikali, tukaomba serikali hawa watu wahamishwe, na mpaka sasa hatujaona hatua yeyote ambayo imefanyika”,aliongeza Mwangi
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

