News
Zaidi ya familia 5,000 zahofia kufurushwa Matuga,Kwale.
Zaidi ya familia elfu 5 eneo la Matuga kaunti ya Kwale zinahofia kufurushwa katika ardhi zao yenye zaidi ya ekari elfu 6.
Ardhi hizo zilikamilisha mda wa malipo ya kodi kwa waekezaji tangu 2011 na kutarajiwa kurejeshewa wakaazi, japo zinadaiwa kuchukuliwa na mabwenyenye katika njia tatanishi.
Wakiongozwa na mwenyekiti wao Mwafitina Juma Bakari wakaazi hao walisema kwamba licha ya tume ya ardhi nchini NLC kuzuru katika ardhi hizo mapema mwaka 2025, hadi sasa hakuna chochote kinachofanyika.
“Block ten kwanza walikuwa wanasema nyumba ni tatu wale mabwenyenye katika historia ambayo iko pale, lakini walipokuja NLC wakazunguka wakaona nyumba zaidi ya 300 wakashanga, halafu block hiyo hiyo tulikuwa tumeandikiwa barua na NCL mwaka 2011 kwamba tupimiwe na tuko na barua, lakini twashangaa mpaka sasa twashangaa haijapimwa na bwenyenye amerejea na kuchukua shamba”, walisema wakaazi.
Wakaazi hao walimtaka Rais Ruto kuingilia kati mzozo huo ili kuhakikisha jamii hizo zinapata haki.
Vile vile walieleza mahangaiko yao na kuashiria kuchoshwa na dhulma za kihistoria za ardhi.
“Watu wapwani tunadhulumika, watu wa Kwale tunadhulumika, watu wa Waa Ng’ombeni tunadhulumika, tunaomba aingilie kati kwa sababu hata hiyo mambo ya blue economy hatuna nafasi nayo kwa sababu mashamba bwenyenye anapima mpaka baharini, sasa hatua sehemu za kuegesha maboti, hatuna lolote”,waliongeza wakaazi.
Waliishikilia kuwa iwapo suala hilo halitaangaziwa huenda wakalazimika kuandamana hadi ofisi kuu za tume ya ardhi NLC jijini Nairobi kudai haki zao.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.
News
Rais Ruto atia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya uwekezaji wa mali
Rais William Ruto ametia saini kuwa sheria mswada wa hazina ya kitaifa ya uwekezaji wa mali (Sovereign Wealth Fund), hatua inayotajwa kuwa muhimu katika juhudi za Kenya za kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kulinda utajiri wa taifa na kuchochea ukuaji wa uchumi wa muda mrefu.
Utiaji huo wa saini ulifanyika katika Ikulu ya Nairobi na unaweka msingi wa kisheria wa kuanzishwa na kusimamiwa kwa mfuko wa taifa wa uwekezaji wa mali na kwamba unatarajiwa kuiwezesha nchi kuhifadhi rasilimali za umma zinazobaki baada ya matumizi ya kawaida, kufadhili uwekezaji wa kimkakati na kuimarisha uwezo wa uchumi kukabiliana na misukosuko ya kifedha siku zijazo.
Sheria hiyo mpya inaleta mfumo rasmi wa usimamizi wa utajiri wa taifa kwa kutenga akiba kwa ajili ya vizazi vijavyo, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili uwekezaji katika miundombinu ya kimkakati ili kuongeza uimara wa kifedha nchini pamoja na kuhimiza matumizi yenye uwajibikaji ya rasilimali za umma.
Mfuko huo utatumika kuwekeza mapato ya ziada yanayotokana na rasilimali za asili na mali nyingine za umma, kwa lengo la kuhakikisha manufaa yake yanawanufaisha wananchi wa sasa na vizazi vijavyo.
Aidha, mfuko huo unakusudia kupunguza athari za changamoto za kiuchumi kwa kutoa kinga ya kifedha wakati wa misukosuko ya uchumi.
Sheria hiyo ni sehemu ya ajenda pana ya serikali ya mageuzi ya uchumi inayolenga kuimarisha usimamizi wa fedha za umma, kuongeza uwazi na kuendeleza maendeleo endelevu.
Pia, sheria hiyo imeweka mfumo wa uongozi na usimamizi wa mfuko huo, ukiwemo utaratibu wa kuhakikisha uwajibikaji, uwazi na usimamizi madhubuti katika uwekezaji na matumizi ya rasilimali za umma.
Maafisa wa serikali wameeleza kuwa Mfuko wa Taifa wa Uwekezaji wa Mali utakuwa na mchango mkubwa katika kufadhili miradi ya maendeleo yenye kipaumbele nchini huku ukihifadhi utajiri wa taifa kwa manufaa ya vizazi vijavyo.
Kupitishwa kwa sheria hiyo kunaiweka Kenya miongoni mwa mataifa yanayoongezeka duniani ambayo yameanzisha mifuko ya taifa ya uwekezaji wa mali kwa lengo la kulinda mali za taifa, kuimarisha uthabiti wa uchumi na kufadhili malengo ya maendeleo ya muda mrefu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
IEBC yakosolewa dhidi ya masharti mapya kwa wanasiasa
Kiongozi wa vijana katika Chama cha Wiper kaunti ya Kwale Nyawa Masai ameikosoa Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC kutokana na masharti mapya iliyotoa dhidi ya wanasaisa kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Nyawa ameitaka Tume hiyo kuzingatia kanuni zake na taratibu za kuandaa uchaguzi na wala sio kila uchao kutoa masharti ambayo yanakinzana na majukumu ya Tume, akisema kuna taasisi zengine za umma zinafaa kuwajibika.
Akizungumza katika mkutano wa kisiasa katika eneo la Mwereni gatuzi dogo la Lungalunga kaunti ya Kwale, Nyawa aliesisitiza haja ya wanasiasa kupewa nafasi ya kuzungumza na wananchi sawa na kueleza sera zao bila ya vizuizi.
Kiongozi huyo wa vijana ambaye alitangaza nia yake ya kuwania kiti cha uwakilishi wadi ya Mwereni wakati wa uchaguzi ujao, amesema taifa la Kenya linazingatia demokrasia na kwamba kila taasisi inafaa kutekeleza majukumu yake.
“Katika uwaja wa siasa IEBC inakuzi moja tu kama msimamizi na kama msimamizi anaanza kutengeza sheria hapo ndipo anakosea, hii Kneya ni nchi ya demokrasia kwa hivyo IEBC isilete sheria nyingi na kufuatilia wanasiasa kuhusu pesa watatumia kwa kampeni, hiyo sio jukumu lake kuna taasisi inaitwa EACC”, alisema Nyawa.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

