News
IEBC yahakikishia wakenya usalama wa taarifa za usajali
Tume uchaguzi na mipaka nchini (IEBC) imerejesha tovuti yake ambayo wapigakura huthibitisha taarifa zao za usajili, baada ya kipindi cha ukarabati.
Hii ni kufuatia malalamishi ya umma kuhusu hitilafu isiyoeleweka ambayo ilisababisha mamilioni ya wakenya kushindwa kupata taarifa zao za usajili kama wapigakura.
Tume hiyo ilitangaza kwamba tovuti hiyo sasa imerejea mtandaoni, kufuatia kipindi cha ukarabati wa mfumo unaolenga kuhamisha miundombinu yake ili kuimarisha utendakazi na usalama.
Tangazo hilo lilifuatia siku za sintofahamu ambapo wakenya hawakuweza kuthibitisha maelezo yao ya usajili, iwe kupitia tovuti ya IEBC au kwa njia ya ujumbe mfupi.
Wapigakura walipata ugumu wa kutuma nambari ya kitambulisho au ya pasipoti pamoja na mwaka wao wa kuzaliwa, kulingana na mahitaji ya IEBC.
Njia zote mbili za uthibitishaji hazikuweza kufikiwa wakati wa ukarabati, na hivyo kusababisha wasiwasi kuongezeka, haswa wakati joto la kisiasa linapozidi kuongezeka kuelekea uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.
Katika taarifa iliyotolewa siku ya Jumapili 6, Julai 2025 bodi ya uchaguzi iliwahakikishia wapiga kura, ikisema, “Tungependa kuwahakikishia wakenya wote kwamba maelezo ya usajili wa wapigakura 22,120,458 waliojiandikisha, kama yalivyorekodiwa wakati wa uchaguzi mkuu wa 2022, yanasalia shwari na salama.
IEBC iliongeza kuwa uboreshaji wa mfumo ulikuwa muhimu ili kuimarisha utoaji wa huduma kupitia utendakazi bora wa mfumo na usalama wa data.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

