News
Mwanaume mmoja ahukumiwa kifungo cha mwaka mmoja gerezani kwa kosa la uvamizi
Mahakama ya Kilifi imemhukumu kifungo cha mwaka mmoja gerezani mwanaume wa umri wa miaka 30 kwa kosa la kuvamia na kumjeruhi mwenzake.
Akitoa hukumu hiyo, Hakimu wa Mahakama hiyo Ivy Wasike amesema hukumu hiyo imezingatia uzito wa kesi hiyo na ushahidi wa pande zote uliotolewa mbele ya Mahakama kuhusu kesi hiyo.
Hukumu hiyo imetolewa baada ya kiongozi wa mashtaka Nancy Njeru kueleza Mahakama kwamba mshtakiwa Kelvin Fujo Magogo ana rekodi ya uhalifu wa wizi wa mifugo na kesi hiyo iko katika Mahakama hiyo.
Awali kabla ya hukumu hiyo kutolewa, Mahakama ilielezwa kwamba mshtakiwa Fujo, mkaazi wa Madamani wadi ya S okoke eneobunge la Ganze kaunti ya Kilifi, mnamo tarehe 14 mwezi Juni mwaka 2022 mwendo wa saa saba usiku katika eneo la Kiwandani mjini Kilifi akitumia panga alimjeruhi mlalamishi Noah Karisa Kalume.
Mahakama hiyo vilevile ilielezwa kwamba mshtakiwa aliabiri pikipiki ya mlalamishi ili kupelekwa kwake ambapo baadaye aliingia ndani ya nyumba kuchukua nauli badala yake akatoka na panga na kumjeruhi mlalamishi ambaye aliokolewa na bodaboda mwenzake aliyekuwa akipita na kumfikisha hosipitalini kwa matibabu.
Mshtakiwa ameelezwa kuwa ana siku 14 za kukata rufaa iwapo hajaridhishwa na hukumu hiyo.
Taarifa ya Teclar Yeri
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

