News
Polisi wanachunguza tukio la mauaji ya Wanawake wanne Kwale
Maafisa wa polisi katika kaunti ya Kwale wameanzisha uchunguzi kuhusu tukio la mauaji ya Wanawake wanne, ndani ya vyumba za wageni katika meneo ya Samburu, Taru na Meli-kubwa.
Kamanda wa Polisi eneo la Samburu Lydia Mumbo alisema ripoti iliyotolewa awali ilionyesha kwamba mshukuwa aliwachukua Wanawake hao kwenye vyumba vya wageni kisha kuwanyonga kabla ya kutoroka.
Lydia alisema mshukiwa huyo pia anadaiwa baada ya kutekeleza kitendo hicho cha kimya alichukua baadhi ya nguo za waathiriwa na kutoroka nazo ili kuficha ushahidi.
“Tumeona hali sasa imeanza kubadilika na kuwa hatari kwa usalama wa wananchi kwani awali jamaa huyo ambaye bado anasakwa na maafisa wa polisi alikuwa ana njama fiche na kuwauwa wanawake hao katika sehemu tofauti”, alisema Lydia.
Aidha aliwataka Wanawake wanaojihusisha biashara ya ngono kuwa waangalifu zaidi huku akiwarai wananchi kushirikiana na maafisa wa usalama katika kutoa taarifa zitakazochangia kutiwa nguvuni kwa mshukiwa huyo.
“Tunawarai wananchi kuchukua tahadhari na kuripoti wahalifu kwa maafisa wa polisi ili hatua za kisheria zichukuliwe mara moja na wananchi pia wawe waangalifu”, aliongeza Kamanda huyo wa Polisi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Wadau wa sekta ya uchukuzi wasitisha mgomo wao
Maafisa wa sekta ya uchukuzi wameahirisha mgomo wao baada ya mazungumzo yaliyoongozwa na Rais William Ruto katika ikulu ya Mombasa.
Maafisa hao wakiongozwa na rais wa Muungano wa wamiliki wa matatu Albert Karagacha wamesema kuwa mengi ya masuala waliokuwa nayo ikiwemo kupanda kwa bei ya mafuta nchini yameangaziwa kwa kina na rais Ruto.
Karagacha amewataka wahudumu wa sekta ya uchukuzi wa umma pamoja na wamiliki wa magari ya uchukuzi wa mizigo kuhakikisha wanarudisha magari yao barabarani, akisema masuala waliowasilisha kwa rais yameangaziwa
Akizungumza mda mfupi baada ya kufanya kikao na rais William Ruto mjini Mombasa, Karagacha amesema serikali imekuwa kiangazia kwa kina masuala mbali mbali yanayohusu sekta ya uchukuzi nchini.
Aidha amesema iwapo bado serikali itakuwa inajikokota katika kufanikisha masuala waliojadiliana basi wataitisha mazungumzo zaidi na Wizara husika ili kuafikiwa kwa ajenda zao huku akisema japo suala la mzozo wa mafuta sio jambo la Kenya pekee lakini taifa inawajibu wa kusaidia wananchi wake.
Wakati huo huo Karagacha amewataka wakenya kutoingiza siasa katika suala la kupanda kwa bei ya mafuta nchini.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mshukiwa wa ulanguzi na usafirishaji wa watoto anyimwa dhamana
Mahakama ya Shanzu imemnyima dhamana mshukiwa wa ulanguzi wa watoto zaidi ya 20.
Mahakama imeagiza mshukiwa huyo kuzuiliwa rumande ili kuwawezesha maafisa wa polisi kukamilisha uchunguzi wao.
Mahakama imeelezwa kwamba mshukiwa huyo Almasi Rama Amos mwenye umri wa miaka 27 alikamatwa na maafisa wa upelelezi kutoka kitengo cha kupambana na ulanguzi wa binadamu na ulinzi wa watoto (AHTCPU) pamoja na maafisa wa idara ya upelelezi wa Jinai kutoka kaunti ya Mombasa.
Kukamatwa kwake kufuatia wiki kadhaa za uchunguzi kuhusu ripoti za unyanyasaji wa watoto zinazowalenga wasichana wadogo walio katika mazingira magumu.
Rama, anayetuhumiwa kwa kujihusisha na kundi linalodaiwa kuwa la ulanguzi wa watoto na dhulma za kingono na kufikishwa katika Mahakama ya Shanzu kufuatia operesheni ya kiusalama iliyoidhinishwa na maafisa hao.
Rama alipatikana katika mtaa wa Nguu Tatu eneo la Concordia katika kaunti ndogo ya Kisauni akiwa na watoto watatu wa kike.
Mahakama imeelezwa kuwa mshukiwa anadaiwa kuendesha “vituo vya uokoaji” katika kaunti za Mombasa na Kilifi kwa kujifanya kuwalea na kuwapa ushauri.
Kulingana na uchunguzi vituo hivyo vilikuwa vikitumika kama msingi wa dhulma za kingono na unyanyasaji wa watoto.
Alipokamatwa, mshukiwa aliwaongoza maafisa hadi kituo chengeni eneo la Ribe katika eneo bunge la Rabai, ambapo maafisa wa upelelezi waliwaokoa watoto 19 wa jinsia ya kike na kufikisha jumla ya waathiriwa waliookolewa kufikia ishirini na wawili (22).
Mbele ya Mahakama ya Shanzu tarehe 21 Mei, 2026, mshukiwa amekabiliwa na mfululizo wa mashtaka, ikiwemo unajisi, biashara ya watoto kwa madhumuni ya kuwadhulumu kingono pamoja na unyanyasaji wa watoto ambapo amekana mashtaka hayo.
Kesi hiyo imepangwa kutajwa Juni 8, 2026.
Taarifa ya Teclar Yeri

