News
Polisi watoa onyo kwa wanyakuzi wa ardhi Kilifi
Idara ya usalama kaunti ya Kilifi imetoa onyo kali kwa wanaoendeleza unyakuzi wa ardhi za umma, ikisema watakabiliwa kikamilifu.
Kamishna wa kaunti ya Kilifi David Wanyonyi ametoa onyo hilo, akizidi kulionya kundi la Team Mashamba dhidi ya tabia hiyo.
Katika kikao na Wanabahari kuhusu usalama wa kaunti ya Kilifi kabla ya ziara ya rais William Ruto ya uzinduzi wa miradi ya maendeleo, Wanyonyi amesema serikali haitalinyamazia suala hilo wakati wananchi wakiendelea kuhangaishwa.
Kamishna Wanyonyi alisema tayari maafisa wa usalama wako nyanjani kuhakikisha usalama unaimarishwa kabla ya ziara ya rais, akiwataka wananchi kuondoa wasiwasi kwani maafisa wa usalama wako imara kulinda mali na raslimali za wananchi.
“Kama maafisa wa usalama tunatoa onyo kwa wavamizi wa mashamba ya umma wakidhani hayatumiki, tunawaambia hiyo tabia waache, hasa hii Team Shamba imekuwa na tabia ya kuvamia mashamba na kugawa, tunawaambia hiyo tabia hatutakubali na kutawakamata”, alisema Wanyonyi.
Aidha alisisitiza kwamba maafisa wa usalama hawatarudi nyuma katika kupambana na walanguzi wa dawa za kulevya kaunti ya Kilifi, akisema watakamatwa na kufikishwa Mahakamani ili kulinda vijana dhidi ya Mihadarati.
“Ni kweli kumekuwa na kesi za Mihadarati, lakini tunasema kwamba kama maafisa wa usalama kwa ushirikiano na vitengo mbalimbali tutahakikisha walanguzi wa Mihadarati wamekamatwa na kufikisha Mahakamani kulingana na sheria’,alisisitiza Wanyonyi.
Ziara ya rais Ruto kanda ya Pwani inatarajiwa kuwa na manafaa makubwa kwa wananchi, huku suala tata la ardhi, likitarajiwa kuangaziwa na wananchi kupewa hati miliki.
News
Baraza la Jamii ya Sekuye lalamikia uchimbaji wa madini kiholela
Baraza la Wazee wa jamii ya Sekuye eneo la Moyale kaunti ya Marsabit limejitokeza na kulalamikia kuharibiwa kwa mazingira ya maeneo yao hasa katika kijiji cha Dabel kutokana na uchimbaji madini kiholela.
Wazee hao wamewalaumu viongozi wao ikiwemo serikali ya kaunti kwa kulinyamazia suala hilo huku wakaazi wakiendelea kunyanyaswa raslimali zao.
Baraza hilo, chini ya Katibu wake mkuu Haji Hassan Tepo, limedai kwamba uchimbaji huo wa madini kiholela, unyakuzi wa ardhi, unyanyasaji wa jamii umechangiwa na baadhi ya wawekezaji kutoka taifa Jirani la Somalia na Ethiopia ambao hawana vibali halali.
Hassan aliimtaka serikali kupitia Waziri wa madini nchini Hassan Ali Joho kuingilia kati suala hilo na kuhakikisha uchumbaji wa madini katika kijiji cha Dabel unasitishwa kwani wawekezaji zaidi ya 20 wamebuni makundi na kuendelea kuwanyanyasa wenyeji.
Hassan aliweka wazi kwamba baraza hilo pamoja na jamii ya Sekuye linapinga mpango huo na kusisitisha kwamba hawatakubali ardhi yao wanayoitegemea kwa shughuli mbalimbali kutumika vibaya.
Naibu Mwenyekiti wa baraza hilo Abdukadir Dilo alisema hali hiyo imewasabibishia hasara kwani mifugo imeangamia, uchumi wa kijiji hicho ukididimia zaidi na akamtaka rais Ruto kuingilia kati kwani licha ya Waziri Murkomen kufunga uchumbaji kufuatia utovu wa usalama bado wawekezaji kutoka Ethiopia na Somali wamekuwa wakiendeleza mpango huo.
Wazee hao hata hivyo walisisitiza kwamba hawatakubali kuachilia ardhi yao kunyakuliwa na watu wanaodai kuwa wawekezaji ilhali vijana wa eneo hilo hawana kazi, huku wanafunzi wakiacha shule na zaidi ya akina mama 22 wakiachwa na wanaume zao kufuatia suala hilo katika kijiji cha Dabel.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Murkomen ahimiza ushirikiano wa pamoja na wadau wa masuala ya ubaharia
Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen, ametoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya washirika na wadau ili kuimarisha usalama wa baharini na maziwa makuu.
Akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi wa kongamano la kamati ya uongozi wa Jukwaa la ushirikiano wa taarifa ya kanda ya Indo-Pasifiki (IORIS) lililofanyika mjini Mombasa, Waziri huyo alisisitiza kuwa ushirikiano wa mapema ni muhimu katika kukabiliana na vitisho vinavyoibuka vya usalama wa baharini.
“Ushirikiano wa mapema na muhimu katika kulinda usalama wetu wa baharini,” alisema Murkomen.
Kongamano hilo la siku tatu linaandaliwa kwa pamoja na huduma ya Walinzi wa Pwani ya Kenya (KCGS) pamoja na mradi wa njia muhimu za baharini wa Indo-Pasifiki unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU-CRIMARIO), ukiwaleta pamoja wadau wa usalama wa baharini..
Mradi wa EU-CRIMARIO umeundwa kuimarisha usalama na ulinzi wa baharini kupitia kuboreshwa kwa ushirikiano wa taarifa na uratibu wa operesheni.

Kongamano la siku tatu la kamati ya uongozi la Jukwaa la ushirikiano wa taarifa ya kanda ya Indo-Pasifiki (IORIS), Mombasa
Mpango wake mkuu, IORIS, ni jukwaa salama na lisiloegemea upande wowote linalotumia mtandao, unaounganisha zaidi ya mashirika 150 kutoka nchi 70, na kuwezesha uratibu wa operesheni za baharini kwa wakati halisi.
Kauli za Murkomen ilijiri kufuatia tangazo la Rais William Ruto kwamba kampuni ya usafiri wa baharini ya Norway, Wilhelmsen, itaajiri mabaharia 1,000 kutoka Kenya, baada ya mazungumzo na kampuni hiyo.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na Mkurugenzi wa EU-CRIMARIO Martin Cauchi Inglott, Mkurugenzi mkuu wa huduma ya walinzi wa Pwani ya Kenya Bruno Shioso, Naibu mkuu wa ujumbe wa umoja wa Ulaya nchini Kenya Ondrej Simek, pamoja na washkadau wengine.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

