News
Odinga awaalika wakenya kwenye kumbukumbu za Sabasaba
Kinara wa chama cha ODM Raila Odinga amewaalika wakenya kujumuika naye kati kumbukumbu za maandamano ya siku ya Sabasaba katika uwanja wa Kamukunji jijini Nairobi.
Odinga alisema hatua hiyo ni kuwakumbuka wale waliopigania mfumo wa vyama vingi nchini ambao kulingana naye mfumo huo ulifaulu japo bado kuna mambo mengi ambayo yanahitaji kulainishwa.
Itakumbukwa kuwa Odinga alikuwa miongoni mwa waliopanga siku ya maandamano ya Sabasaba ya kwanza nchini, mnamo Julai 7, 1990.
Odinga alisema yuko tayari kuadhimisha miaka 35 ya siku hii.
Kinara huyo wa ODM alisema uwanja wa Kamukunji jijini Nairobi umebeba historia ya kipekee kutokana na matukio ya wakati huo, ambapo waliowasili katika Sabasaba ya kwanza walikabiliwa na maafisa wa usalama, baadhi walipoteza maisha na mamia wakijeruhiwa katika vita vya kupigania siasa za vyama vingi.
Wakati huo huo kundi la wahuni lilivamia kikao kilichokuwa kikihutubiwa na makundi ya kinamama katika ofisi za tume ya kutetea haki za kibinadam KHRC Jijini Nairobi jumapili 6, Julai 2025.
Kinamama hao walikuwa wamewasili katika ofisi za tume hiyo ili kuzungumzia siku ya Sabasaba na walilazimika kusitisha kikao hicho huku mali na bidhaa nyingine muhimu zikiibwa.

Baadhi ya wanawake waliovamiwa katika makao makuu ya tume ya KHRC Nairobi
Wanahabari waliokuwa sehemu hiyo pia walivamiwa na kukimbilia usalama wao huku kinamama hao wakilazimika kuandaa kikao hicho sehemu tofauti baadaye.
Hata hivyo tume hiyo ya KHRC ililaani tukio hilo na kumtaka inspekta jenerali wa polisi nchini Douglas Kanja kufanya uchunguzi na kuwakamata waliohusika na uvamizi huo
Taarifa ya Joseph Jira
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

