News
Uhaba wa maji wakera wakaazi Mombasa
Wakaazi wa mtaa wa mabanda wa Bangladeshi eneo bunge la Jomvu, kaunti ya Mombasa, wanalalamikia uhaba mkubwa wa maji unaoendelea kushuhudiwa kwa zaidi ya mda wa wiki tatu sasa.
Wakiongozwa na Betty Achieng’, wakaazi hao walisema hali hiyo imeathiri pakubwa shughuli zao za kila siku.
Walisema bei ya maji imeongezeka mara dufu kutokana na uhaba huo.
Aidha walisema wanalazimika kununua maji kutoka kwa wauzaji wa rejareja, wanaotumia mikokoteni huku wakihofia usalama wa maji hayo, hasa katika matumizi ya nyumbani.
“Tunaomba msaada kwa serikali itusaidie kwa mambo ya maji, angalia vile tunahangaika hata kazini hatuendi kwa sababu vitu vyetu ni vichafu, tuko na watoto wadogo, nguo ni chafu, saa zingine tunakaa hapa tunakaa hapa tunangoja msaada wa maji”, walisema wakaazi hao
Kwa upande wao, maafisa kutoka wizara ya maji ya kaunti ya Mombasa walieleza kuwa tatizo hilo linatokana na upungufu wa maji katika kituo cha kusambaza maji cha Baricho kaunti ya Kilifi, hali iliyosababisha maeneo mengi ya kaunti hiyo kukosa bidhaa hiyo muhimu.
Taarifa ya Mwanahabari wetu.
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

