News
Wanaharakati wanataka barabara ya Mombasa-Malindi kukamilishwa kujengwa
Wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu katika eneo la Pwani wamefanya maandamano ya amani wakilalamikia hali mbovu ya barabara ya Mombasa-Malindi.
Wanaharakati hao wanasema ukarabati wa barabara hiyo hasa eneo la Mtwapa umechukua muda mrefu kukamilika na kuchangia kudorora kwa uchumi wa eneo la Pwani huku magari yanayotumia barabara hiyo yakiendelea kuharibika kila mara.
Wakiongozwa na Mkurugenzi mkuu wa Shirika la Vocal Africa Hussein Khalid, Wanaharakati hao walikosoa mwendo wa polepole wa ujenzi wa barabara hiyo, wakisema umegeuka kuwa tishio kwa usalama na shughuli za kiuchumi.
“Kila kukicha magari yanaharibika barabara ni mbovu, kwa hivyo tunaiambia serikali tunataka hii barabara iishe haraka iwezekanavyo”, alisema Khalid.

Wanaharakari wafunga barabara ya Mombasa -Malindi wakilalamikia ubovu wa barabara hiyo
Kwa upande wake, Khelef Khalifa wa shirika la MUHURI amekosoa jinsi miradi ya maendeleo katika eneo la Pwani inavyotekelezwa kwa mwendo wa kujikokota, akisema hali hiyo imelemaza utoaji wa huduma muhimu kwa wananchi.
“Tukienda Feri, watu ambao wanavuka kwa feri ni laki nne kwa siku na magari elfu 20, hakuna daraja kila kitu kinatoka hapa kinafanywa huko kila kitu kinafanywa huko polisi wenyewe wanalalamika ni utovu wa usalama sasa tumeanza kupeleka barua wanaanza kujazajaza kwa mawe”, alisema Khelef
Wanaharakati hao sasa wanaitaka serikali kuharakisha ukamilishaji wa barabara hiyo ili kupunguza ajali, msongamano wa magari pamoja na kuboresha shughuli za biashara kati ya kaunti za Pwani
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Baraza la Jamii ya Sekuye lalamikia uchimbaji wa madini kiholela
Baraza la Wazee wa jamii ya Sekuye eneo la Moyale kaunti ya Marsabit limejitokeza na kulalamikia kuharibiwa kwa mazingira ya maeneo yao hasa katika kijiji cha Dabel kutokana na uchimbaji madini kiholela.
Wazee hao wamewalaumu viongozi wao ikiwemo serikali ya kaunti kwa kulinyamazia suala hilo huku wakaazi wakiendelea kunyanyaswa raslimali zao.
Baraza hilo, chini ya Katibu wake mkuu Haji Hassan Tepo, limedai kwamba uchimbaji huo wa madini kiholela, unyakuzi wa ardhi, unyanyasaji wa jamii umechangiwa na baadhi ya wawekezaji kutoka taifa Jirani la Somalia na Ethiopia ambao hawana vibali halali.
Hassan aliimtaka serikali kupitia Waziri wa madini nchini Hassan Ali Joho kuingilia kati suala hilo na kuhakikisha uchumbaji wa madini katika kijiji cha Dabel unasitishwa kwani wawekezaji zaidi ya 20 wamebuni makundi na kuendelea kuwanyanyasa wenyeji.
Hassan aliweka wazi kwamba baraza hilo pamoja na jamii ya Sekuye linapinga mpango huo na kusisitisha kwamba hawatakubali ardhi yao wanayoitegemea kwa shughuli mbalimbali kutumika vibaya.
Naibu Mwenyekiti wa baraza hilo Abdukadir Dilo alisema hali hiyo imewasabibishia hasara kwani mifugo imeangamia, uchumi wa kijiji hicho ukididimia zaidi na akamtaka rais Ruto kuingilia kati kwani licha ya Waziri Murkomen kufunga uchumbaji kufuatia utovu wa usalama bado wawekezaji kutoka Ethiopia na Somali wamekuwa wakiendeleza mpango huo.
Wazee hao hata hivyo walisisitiza kwamba hawatakubali kuachilia ardhi yao kunyakuliwa na watu wanaodai kuwa wawekezaji ilhali vijana wa eneo hilo hawana kazi, huku wanafunzi wakiacha shule na zaidi ya akina mama 22 wakiachwa na wanaume zao kufuatia suala hilo katika kijiji cha Dabel.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Murkomen ahimiza ushirikiano wa pamoja na wadau wa masuala ya ubaharia
Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen, ametoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya washirika na wadau ili kuimarisha usalama wa baharini na maziwa makuu.
Akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi wa kongamano la kamati ya uongozi wa Jukwaa la ushirikiano wa taarifa ya kanda ya Indo-Pasifiki (IORIS) lililofanyika mjini Mombasa, Waziri huyo alisisitiza kuwa ushirikiano wa mapema ni muhimu katika kukabiliana na vitisho vinavyoibuka vya usalama wa baharini.
“Ushirikiano wa mapema na muhimu katika kulinda usalama wetu wa baharini,” alisema Murkomen.
Kongamano hilo la siku tatu linaandaliwa kwa pamoja na huduma ya Walinzi wa Pwani ya Kenya (KCGS) pamoja na mradi wa njia muhimu za baharini wa Indo-Pasifiki unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU-CRIMARIO), ukiwaleta pamoja wadau wa usalama wa baharini..
Mradi wa EU-CRIMARIO umeundwa kuimarisha usalama na ulinzi wa baharini kupitia kuboreshwa kwa ushirikiano wa taarifa na uratibu wa operesheni.

Kongamano la siku tatu la kamati ya uongozi la Jukwaa la ushirikiano wa taarifa ya kanda ya Indo-Pasifiki (IORIS), Mombasa
Mpango wake mkuu, IORIS, ni jukwaa salama na lisiloegemea upande wowote linalotumia mtandao, unaounganisha zaidi ya mashirika 150 kutoka nchi 70, na kuwezesha uratibu wa operesheni za baharini kwa wakati halisi.
Kauli za Murkomen ilijiri kufuatia tangazo la Rais William Ruto kwamba kampuni ya usafiri wa baharini ya Norway, Wilhelmsen, itaajiri mabaharia 1,000 kutoka Kenya, baada ya mazungumzo na kampuni hiyo.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na Mkurugenzi wa EU-CRIMARIO Martin Cauchi Inglott, Mkurugenzi mkuu wa huduma ya walinzi wa Pwani ya Kenya Bruno Shioso, Naibu mkuu wa ujumbe wa umoja wa Ulaya nchini Kenya Ondrej Simek, pamoja na washkadau wengine.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

