News
Baadhi ya Wananchi wanataka walipwe kujisajili kuwa wapiga kura
Afisa wa usajili wa tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC eneo bunge la Kilifi Kaskazini kaunti ya Kilifi , John Mwawasi amesema wanapania kusajili wapiga kura wapya 13,316 katika zoezi hilo ambalo linakamilika leo Aprili 28 baada ya kuanza Machi 30.
Katika mazungumzo ya kipekee na Coco FM kwenye afisi za IEBC hapa mjini Kilifi, Mwawasi alisema kufikia Aprili 27 walikuwa wamefanikiwa kusajili wapiga kura wapya 12,999 na kwamba muda wa usajili hautaongezwa baada ya kukamilika leo.
“Itakuwa vyema kama wakenya watajitokeza kwa wingi kabla ya zoezi hili kukamilika kwani IEBC haitaongeza muda licha ya Viongozi na baadhi ya wananchi kupendekeza muda zaidi kuongezwa” alisema Mwawasi.
Mwawasi alisema vijana wengi walijitokeza katika zoezi hilo huku akitaja baadhi ya changamoto ambazo wamezipitia katika usajili wa wapiga kura wapya.
“Baadhi ya wananchi hasa vijana wanalalamikia ukosefu wa vitambulisho na wengine kutaka kulipwa ili kujisajili kuwa wapiga kura”Aliongeza Mwawasi
Mwawasi pia alisema usajili wa wapiga kura utaendelezwa katika afisi za IEBC na vituo vya Huduma Center.

Wakaazi wa Kilifi Kazkazini wakishiriki zoezi la usajili wa wapiga kura
Kwa upande wa wananchi ambao walifika katika afisi za IEBC Kilifi Kaskazini walieleza namna zoezi hilo lilikuwa huku wakitoa wito kwa wakenya wengine kujisajili kwa wingi kuwa wapiga kura ili washiriki uchaguzi mkuu ujao wa mwaka wa 2027.
Haya yanajiri huku Tume (IEBC) ikifanya kila juhudi kufikia azma yake ya kuwaandikisha wapiga kura wapya milioni 2.5 na kaunti za Nairobi na Kiambu zinaongoza kwa idadi ya juu ya wapiga kura wapya.
Kaunti za Lamu, Isiolo na Mandera zikiandikisha idadi ya chini ya waliojisajili.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Wadau wa sekta ya uchukuzi wasitisha mgomo wao
Maafisa wa sekta ya uchukuzi wameahirisha mgomo wao baada ya mazungumzo yaliyoongozwa na Rais William Ruto katika ikulu ya Mombasa.
Maafisa hao wakiongozwa na rais wa Muungano wa wamiliki wa matatu Albert Karagacha wamesema kuwa mengi ya masuala waliokuwa nayo ikiwemo kupanda kwa bei ya mafuta nchini yameangaziwa kwa kina na rais Ruto.
Karagacha amewataka wahudumu wa sekta ya uchukuzi wa umma pamoja na wamiliki wa magari ya uchukuzi wa mizigo kuhakikisha wanarudisha magari yao barabarani, akisema masuala waliowasilisha kwa rais yameangaziwa
Akizungumza mda mfupi baada ya kufanya kikao na rais William Ruto mjini Mombasa, Karagacha amesema serikali imekuwa kiangazia kwa kina masuala mbali mbali yanayohusu sekta ya uchukuzi nchini.
Aidha amesema iwapo bado serikali itakuwa inajikokota katika kufanikisha masuala waliojadiliana basi wataitisha mazungumzo zaidi na Wizara husika ili kuafikiwa kwa ajenda zao huku akisema japo suala la mzozo wa mafuta sio jambo la Kenya pekee lakini taifa inawajibu wa kusaidia wananchi wake.
Wakati huo huo Karagacha amewataka wakenya kutoingiza siasa katika suala la kupanda kwa bei ya mafuta nchini.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mshukiwa wa ulanguzi na usafirishaji wa watoto anyimwa dhamana
Mahakama ya Shanzu imemnyima dhamana mshukiwa wa ulanguzi wa watoto zaidi ya 20.
Mahakama imeagiza mshukiwa huyo kuzuiliwa rumande ili kuwawezesha maafisa wa polisi kukamilisha uchunguzi wao.
Mahakama imeelezwa kwamba mshukiwa huyo Almasi Rama Amos mwenye umri wa miaka 27 alikamatwa na maafisa wa upelelezi kutoka kitengo cha kupambana na ulanguzi wa binadamu na ulinzi wa watoto (AHTCPU) pamoja na maafisa wa idara ya upelelezi wa Jinai kutoka kaunti ya Mombasa.
Kukamatwa kwake kufuatia wiki kadhaa za uchunguzi kuhusu ripoti za unyanyasaji wa watoto zinazowalenga wasichana wadogo walio katika mazingira magumu.
Rama, anayetuhumiwa kwa kujihusisha na kundi linalodaiwa kuwa la ulanguzi wa watoto na dhulma za kingono na kufikishwa katika Mahakama ya Shanzu kufuatia operesheni ya kiusalama iliyoidhinishwa na maafisa hao.
Rama alipatikana katika mtaa wa Nguu Tatu eneo la Concordia katika kaunti ndogo ya Kisauni akiwa na watoto watatu wa kike.
Mahakama imeelezwa kuwa mshukiwa anadaiwa kuendesha “vituo vya uokoaji” katika kaunti za Mombasa na Kilifi kwa kujifanya kuwalea na kuwapa ushauri.
Kulingana na uchunguzi vituo hivyo vilikuwa vikitumika kama msingi wa dhulma za kingono na unyanyasaji wa watoto.
Alipokamatwa, mshukiwa aliwaongoza maafisa hadi kituo chengeni eneo la Ribe katika eneo bunge la Rabai, ambapo maafisa wa upelelezi waliwaokoa watoto 19 wa jinsia ya kike na kufikisha jumla ya waathiriwa waliookolewa kufikia ishirini na wawili (22).
Mbele ya Mahakama ya Shanzu tarehe 21 Mei, 2026, mshukiwa amekabiliwa na mfululizo wa mashtaka, ikiwemo unajisi, biashara ya watoto kwa madhumuni ya kuwadhulumu kingono pamoja na unyanyasaji wa watoto ambapo amekana mashtaka hayo.
Kesi hiyo imepangwa kutajwa Juni 8, 2026.
Taarifa ya Teclar Yeri

