News
Bei ya Mafuta yapandisha joto la kisiasa nchini
Mjadala kuhusu kupanda kwa bei ya mafuta ya petroli nchini Kenya unaendelea kushika kasi, huku wananchi wengi wakitaka maelezo ya kina kuhusu vigezo vinavyotumika kuongeza bei hizo karibu kila mwezi.
Wadau wengi wameonyesha wasiwasi wao kuhusu tofauti ya bei ya mafuta kati ya Kenya na mataifa jirani yasiyo na bandari kama Uganda, Rwanda na Burundi, hali ambayo imeibua maswali kuhusu mfumo wa uagizaji na usimamizi wa mafuta nchini.
Shinikizo hilo limechochea maandamano ya wahudumu wa matatu na baadhi ya washikadau wa sekta ya uchukuzi katika maeneo tofauti nchini leo Mei 18, huku baadhi ya barabara zikishuhudia usumbufu mkubwa wa usafiri.
Akizungumza katika mahojiano na kituo cha runinga nchini, Waziri wa Hazina ya Kitaifa, John Mbadi, alikosoa maandamano hayo akisema hayatoi suluhu ya kudumu kwa changamoto iliyopo.
Kwa mujibu wa Mbadi, hali ya sasa ya bei ya mafuta imeathiriwa kwa kiwango kikubwa na mvutano wa kimataifa unaohusisha Marekani, Israel na Iran, ambao umechangia kuyumba kwa soko la mafuta duniani.
“Maandamano haya hayawezi kushusha bei ya mafuta. Serikali inaendelea kutafuta njia mbadala za kudhibiti gharama hizi,” alisema Mbadi.
Aidha, Waziri huyo aliwashutumu baadhi ya wanasiasa kwa kile alichodai ni kutumia suala la bei ya mafuta kujijenga kisiasa badala ya kutafuta suluhu ya pamoja.
Hata hivyo, serikali bado haijaweka wazi iwapo ongezeko jipya la bei limetokana na shehena mpya ya mafuta iliyowasili nchini mwezi Aprili au changamoto za kimkakati katika uhifadhi wa mafuta nchini Kenya.
Mbadi alisema serikali imekuwa ikitekeleza hatua mbalimbali za kupunguza makali ya ongezeko hilo, zikiwemo:
Kuagiza mafuta kutoka mataifa tofauti
Kutumia mfumo wa serikali kwa serikali (G-to-G)
Kupunguza baadhi ya ushuru wa mafuta
Kupunguza Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT)
Wakati huo huo, serikali imetangaza kikao cha dharura kitakachowakutanisha Waziri wa Kawi, Opiyo Wandayi, Waziri wa Barabara na Uchukuzi, Davis Chirchir, viongozi wa vyama vya uchukuzi pamoja na wadau wengine muhimu katika sekta hiyo.
Lengo la kikao hicho ni kutafuta mwafaka wa haraka wa kusitisha maandamano yanayoendelea huku serikali ikitafuta mbinu za muda mrefu za kudhibiti bei ya mafuta na kupunguza mzigo kwa wananchi.
Taarifa ya Elizabeth Mwende
News
Wadau wa sekta ya uchukuzi wasitisha mgomo wao
Maafisa wa sekta ya uchukuzi wameahirisha mgomo wao baada ya mazungumzo yaliyoongozwa na Rais William Ruto katika ikulu ya Mombasa.
Maafisa hao wakiongozwa na rais wa Muungano wa wamiliki wa matatu Albert Karagacha wamesema kuwa mengi ya masuala waliokuwa nayo ikiwemo kupanda kwa bei ya mafuta nchini yameangaziwa kwa kina na rais Ruto.
Karagacha amewataka wahudumu wa sekta ya uchukuzi wa umma pamoja na wamiliki wa magari ya uchukuzi wa mizigo kuhakikisha wanarudisha magari yao barabarani, akisema masuala waliowasilisha kwa rais yameangaziwa
Akizungumza mda mfupi baada ya kufanya kikao na rais William Ruto mjini Mombasa, Karagacha amesema serikali imekuwa kiangazia kwa kina masuala mbali mbali yanayohusu sekta ya uchukuzi nchini.
Aidha amesema iwapo bado serikali itakuwa inajikokota katika kufanikisha masuala waliojadiliana basi wataitisha mazungumzo zaidi na Wizara husika ili kuafikiwa kwa ajenda zao huku akisema japo suala la mzozo wa mafuta sio jambo la Kenya pekee lakini taifa inawajibu wa kusaidia wananchi wake.
Wakati huo huo Karagacha amewataka wakenya kutoingiza siasa katika suala la kupanda kwa bei ya mafuta nchini.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mshukiwa wa ulanguzi na usafirishaji wa watoto anyimwa dhamana
Mahakama ya Shanzu imemnyima dhamana mshukiwa wa ulanguzi wa watoto zaidi ya 20.
Mahakama imeagiza mshukiwa huyo kuzuiliwa rumande ili kuwawezesha maafisa wa polisi kukamilisha uchunguzi wao.
Mahakama imeelezwa kwamba mshukiwa huyo Almasi Rama Amos mwenye umri wa miaka 27 alikamatwa na maafisa wa upelelezi kutoka kitengo cha kupambana na ulanguzi wa binadamu na ulinzi wa watoto (AHTCPU) pamoja na maafisa wa idara ya upelelezi wa Jinai kutoka kaunti ya Mombasa.
Kukamatwa kwake kufuatia wiki kadhaa za uchunguzi kuhusu ripoti za unyanyasaji wa watoto zinazowalenga wasichana wadogo walio katika mazingira magumu.
Rama, anayetuhumiwa kwa kujihusisha na kundi linalodaiwa kuwa la ulanguzi wa watoto na dhulma za kingono na kufikishwa katika Mahakama ya Shanzu kufuatia operesheni ya kiusalama iliyoidhinishwa na maafisa hao.
Rama alipatikana katika mtaa wa Nguu Tatu eneo la Concordia katika kaunti ndogo ya Kisauni akiwa na watoto watatu wa kike.
Mahakama imeelezwa kuwa mshukiwa anadaiwa kuendesha “vituo vya uokoaji” katika kaunti za Mombasa na Kilifi kwa kujifanya kuwalea na kuwapa ushauri.
Kulingana na uchunguzi vituo hivyo vilikuwa vikitumika kama msingi wa dhulma za kingono na unyanyasaji wa watoto.
Alipokamatwa, mshukiwa aliwaongoza maafisa hadi kituo chengeni eneo la Ribe katika eneo bunge la Rabai, ambapo maafisa wa upelelezi waliwaokoa watoto 19 wa jinsia ya kike na kufikisha jumla ya waathiriwa waliookolewa kufikia ishirini na wawili (22).
Mbele ya Mahakama ya Shanzu tarehe 21 Mei, 2026, mshukiwa amekabiliwa na mfululizo wa mashtaka, ikiwemo unajisi, biashara ya watoto kwa madhumuni ya kuwadhulumu kingono pamoja na unyanyasaji wa watoto ambapo amekana mashtaka hayo.
Kesi hiyo imepangwa kutajwa Juni 8, 2026.
Taarifa ya Teclar Yeri

