News
Mwili wa mtoto Keziah wasafirishwa Tarasaa kaunti ya Tanariver kwa mazishi
Jamaa na Marafiki walifika eneo la Mwezang’ombe kaunti ya Kilifi kuuaga mwili wa Kezia Matuki mwenye umri wa miaka saba na aliyekuwa mwanafunzi wa gredi ya pili ambaye mwili wake ulipatikana wiki chache zilizopita ukiwa umetupwa nje ya boma lao eneo hilo la Kwa Nzai, kabla ya kuusafirisha kwa ajili ya mazishi ambayo yameratibiwa kufanyika Jumamosi 16, Mei 2026 katika eneo la Tarasaa kaunti ya Tana River.
Waliotoa rambirambi zao kwa familia walilaani kitendo hicho, wakimtaja Keziah kama mtoto ambaye alikuwa akishirikiana na watoto wenzake vyema akiwa shuleni na hata nyumbani.
Vilevile, walisema kifo kimezima ndoto ya Kezia ambaye alikuwa mwanafunzi mwenye bidii shuleni.
“Kezia atakumbukwa na wengi kutokana na ucheshi wake na namna alivyokuwa akiiishi na watoto wenzake na hatujawahi kuskia ripoti zozote mbaya kumhusu kama za kuwachokoza wenzake” walisema waombolezaji

Mwili wa Keziah Matuki unaombolezwa na wengi kufuatia kifo chake tatanishi
Kwa upande wake naibu gavana wa kaunti ya Kilifi Flora Chibule alilaani kitendo cha kuuawawa kwa Kezia na kutaka uchunguzi kuharakishwa ili haki ipatikame kwa familia na aliyehusika akabiliwe kisheria.
“Hili ni kisa cha kusikitisha Sana na asasi husika zinapaswa kuharakisha uchunguzi na aliyehusika awajibishwe kisheria ili iwe funzo kwa wengine” Alisema Chibule
Awali ripoti ya upasuaji wa mwili wa Keziah ulibaini kuwa aliuawa kwa kunyongwa.
Ripoti hiyo pia ilibaini kuwa alivunjwa shingo na kisha kunajisiwa.
Daktari mkuu wa hospitali ya rufaa ya Kilifi, Gilbert Angore, alisema sampuli zaidi zilipelekwa katika maabara ya serikali kwa uchunguzi wa kina.
Haya yanajiri huku mshukiwa wa mauaji hayo Dennis Otieno Oduor akiendelea kuzuiliwa rumande huko Shimo la Tewa kaunti ya Mombasa, uchunguzi unapoendelezwa.
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Mbunge wa Nyali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila
Mbunge wa Nyali kaunti ya Mombasa Mohamed Ali amepuzilia mbali madai ya kuhusishwa na siasa za ukabila kwenye kaunti hiyo, akisema anafanya siasa zake bila kujali dini, kabila au hata eneo.
Akizungumza huko Nyali, Ali alisema kuna baadhi ya viongozi katika kaunti ya Mombasa, ambao wamekuwa wakiendekeza propaganda za kumhusisha na siasa za migawanyiko ili kumharibia jina taifa linapojiandaa kwa uchaguzi mkuu ujao wa 2027.
Ali ambaye alitangaza kuwania wadhifa wa ugavana kaunti ya Mombasa, aliwataka viongozi kufanya siasa zao kwa kunadi sera zao kwa wakaazi na maendeleo ambayo watatekeleza na sio kutumia suala la ukabila kuwachafulia wengine jina.
“2017 hakuna mtu aliniita mkabila, 2022 hakuna mtu aliniita mkabila, 2027 wanasema Mohamed Ali ni mkabila.Mimi Mohamed Ali, mimi nauliza nikisimama hapa juu ya gari, niseme kabila zote za Kenya wanaweza pewa nafasi ya ugavana ni kuna makosa?,basi sasa wanazunguka wakisema Mohamed ni mkabila kwasababu ameanza kufungua watu macho’’ alisema Ali.
Aidha, Ali alisema ataendelea kuzuru maeneo mbalimbali ya kauti ya Mombasa kunadi sera zake na kuwataka wakaazi wa kaunti hiyo kuwachagua viongozi wanaofaa ambao wataimarisha kaunti hiyo kimaendeleo.
‘’Mimi nimewaambia nitatembea hii Mombasa kwa uwezo wake mwenyezi mungu kutetea wananchi wa Mombasa’’ aliongeza Ali
Taarifa ya Janet Mumbi
News
Wakimbizi nusu milioni wakabiliwa na baa la njaa, Dadaab
Ripoti iliyotolewa hivi karibu na Shirika la Chakula duniani WFP ilionyesha kwamba zaidi ya wakimbizi nusu milioni wanaoishi katika kambi za wakimbizi za Kakuma na Dadaab zilizoko nchini Kenya, wako katika hatari ya kuangamia kutokana na baa la njaa.
Kambi hizi ambazo zinahifadhi wakimbizi wengi zaidi kutoka nchini Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na Somalia, ziko hatari iwapo zitakosa misaada ya chakula.
Kufuatia hali hiyo ambayo pia imechangiwa na mashirika ya kimataifa kusitisha ufadhili, sasa hali huenda ikawa tofauti baada ya taifa la Korea kwa ushirikiano na Kenya kutoa ufadhili wa shehena ya nafaka ya zaidi ya tani elfu 10 ambayo inakadiriwa kuwa kima cha shilingi milioni 1.2.
Katibu katika Idara ya uhamiaji nchini Belio Kipsang, aliyepokea msaada huo wa Chakula mjini Mombasa na kuhifadhiwa katika maghala ya Shirika la WFP, ameonya kwamba iwapo Kenya itakosa kupokea msaada kutoka kwa washirika na wafadhili wengine, basi italazimika kuchukua maamuzi magumu, ikiwemo kuwaondoa baadhi ya wakimbizi.
“Nyuma ya kila takwimu kuna familia ambazo ustahimilivu wao unaendelea kujaribiwa kila siku: akina mama wanaokosa kula ili watoto wao wapate chakula, watu walio katika mazingira hatarishi wakiruka milo, na vijana wanaokabiliwa na mustakabali usio na uhakika. Hizi si takwimu za kufikirika. Zinawakilisha watu halisi ambao heshima yao, afya yao na matarajio yao ya maisha yanategemea maamuzi tunayofanya kwa pamoja,” alisema.
Wakati wa hafla hiyo ya kupokea msaada huo wa chakula kwa wakimbizi wa Kakuma na Dadaab, Mkurugenzi wa Shirika la WFP nchini Kenya Betty Ka, alisema shehena ya nafaka itasaidia kuwahudumia takribani wakimbizi nusu milioni katika miezi ijayo.
“Usafirishaji huu unaonyesha umuhimu wa ushirikiano imara katika mnyororo wa ugavi wa misaada ya kibinadamu, ambapo ushirikiano huu kati ya Kenya, Mamlaka ya bandari Kenya (KPA), Shirika la viwango la Kenya(KEBS) na mpango wa Chakula Duniani (WFP) kwa kuhakikisha kwamba chakula cha msaada kinafanikishwa”,alisema Betty.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

