News
Jubilee yaunga mkono maandamano ya kupinga bei ya mafuta
Kufuatia sakata ya uagizaji wa mafuta ghushi nchini, sasa Muungano wa upinzani umetishia kufanya maandamano kuanzia wiki ijayo.
Mwenyekiti wa kitaifa wa Chama cha Jubilee Vincent Kemosi, alisema maandamano hayo yanalenga kushinikiza kupunguzwa kwa bei ya mafuta nchini, akimshtumu Rais William Ruto kwa kuchangia mahangaiko wakenya.
Katika kikao na Wanahabari mjini Kilifi kaunti ya Kilifi baada ya kufanya kifanya kikao na viongozi wa chama hicho kanda ya Pwani, Kemosi aliikosoa serikali, akisema wakenya wamechoka kudanganywa na serikali iliyofeli kutekeleza ahadi zake.
“Serikali imeonyesha kushindwa kutatua suala la mafuta na imeonyesha wazi kwamba imefeli, huezi badilisha ushuru wa mafuta baada ya wananchi kulalamika mbona hakufanya hivyo tangu mwanzo, wakenya wamechoka”, alisema Kemosi.
Kemosi, amepinga mpango wa kugawa maeneo kisiasa yaani Zoning, akisema Viongozi wa Chama cha Jubilee watazingatia haki na usawa pamoja na kuandaa uchaguzi wa mashinani wa viongozi wa chama hicho, kauli iliyoungwa mkono na Mwenyekiti wa chama hicho kaunti ya Kilifi Anthony Kingi.
“Katika ya Kenya haijasema mambo ya Zoning, kila mtu ana haki ya kupigania wadhfa anataka, na sisi kama Chama cha Jubilee hatuingi mkono mambo ya zoning, tutahakikisha uchaguzi unafanyika mashinani kwa haki na uwazi”aliongeza Kemosi.

Viongozi wa Chama cha Jubilee wakiongozwa na Mwenyekiti wa kitaifa wa Chama hicho wafanya mkutano wa kuimarisha chama mashinani, Kilifi
Viongozi hao pia waliwarai wananchi kutathmini viongozi wao na kujiunga na vyama vinavyozingatia haki na usawa, wakisisitiza kuunga mkono upinzani.
Katika swala la raslimali, viongozi hao wameshtumu kutengwa kwa raslimali za Pwani hasa zao la mzani na mkorosho, wakisema wakati umefika kwa mpwani kutambulika na raslimali zake kuthaminiwa.
“Zao la Mnazi na Mkorosho ambayo ndio raslimali ya mpwani imetengwa tangu taifa ipate uhuru ndio sisi tunasema ni lazima raslimali ya mpwani pia nayo itambulike kikamilifu”, alisema Garama.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi.
News
Meli yenye bendera ya Kenya yazuiliwa Tanzania
Mamlaka ya usafiri wa majini nchini (KMA), imethibitisha kupokea taarifa kuhusu kuzuiliwa kwa meli yenye bendera ya Kenya katika nchi ya Tanzania.
Kupitia taarifa kwa vyombo vya habari, KMA imesema meli hiyo inayojulikana kama MV SEA MFALME kwa sasa inashikiliwa nchini humo.
Maafisa wa Mamlaka hiyo, wale wa ujasusi, na wanajeshi wa majini wameanzisha uchunguzi kubaini sababu za tukio hilo, na kama meli hiyo ilikuwa imebega shehena gani ndiposa ikazuiliwa.
Mamlaka hiyo imeeleza kuwa inashirikiana kwa karibu na mashirika ya kiserikali pamoja na wadau katika nchi zote mbili ili kubaini kilichosababisha kuzuiliwa kwa meli hiyo na kuhakikisha hatua stahiki zinachukuliwa.
Mamlaka hiyo ilielezwa kwamba tayari imeijulisha Wizara ya masuala ya kigeni nchini inayoongozwa na Waziri Musalia Mudavadi ili kusaidia katika masuala ya kidiplomasia kwani hatua hiyo huenda ikachangia sintofahamu za kimataifa.
KMA imewahakikishia wadau wa sekta hiyo na wamiliki wa meli hiyo kuwa suala hilo linashughulikiwa kwa kufuata taratibu za kisheria na ushirikiano wa kimataifa, na kwamba taarifa zaidi zitatolewa kadri uchunguzi unavyoendelea.
“Tunashirikiana na wadau mbalimbali kwa kuzingatia sheria za kimataifa na ushirikiano wa kidiplomasia kuhusu suala hilo na kwamba hatua za kisheria zitachukuliwa”, alieleza afisa mmoja wa Mamlaka hiyo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Naibu rais akosoa upinzani kuhusu bei ya mafuta nchini
Naibu rais Profesa Kithure Kindiki amerejea tena kaunti ya Kilifi ndani ya kipindi cha mwezi mmoja kuendeleza ziara yake ya kukagua miradi ya maendeleo katika kanda ya Pwani.
Hata hivyo ziara hiyo imeonekana kuangazia zaidi suala tata la kupanda kwa bei ya mafuta nchini ambalo linadaiwa kusababishwa na vita vinavyoendelea katika mashariki ya Kati.
Akitetea hatua ya serikali, naibu rais alisema tayari serikali imechukua hatua madhubuti na za haraka kupunguza ushuru wa mafuta, ili kumkinga mwananchi kutokana na athari za mfumuko wa bei za bidhaa na kuongezeka kwa gharama ya maisha.
Akihutubiwa wananchi katika eneo bunge la Rabai, Professa Kindiki alionekana kuulenga upinzani kwa kuingiza siasa katika suala la mafuta, akikosoa mpango wao wa kuandaa maandamano akisema sio suluhu kwa tatizo hilo.
Hatua ya hii ya Kindiki ilionekana kupokea msukumo kutoka kwa viongozi wakuu ndani chama cha UDA wakiongozwa na katibu wa Chama Omar Hassan Sarai ambaye alikosoa mpango ya upinzani kuandaa maandamano.
Jumatano ya aprili 15, 2026, Rais William Ruto alitangazi mipango ya serikali kutatua tatizo la kupanda kwa bei ya mafuta nchini kwa kupunguza ushuru wa mafuta.
Viongozi wengine walioandamana na naibu rais katika eneo bunge la Rabai akiwemo mwenyekiti wa bodi ya barabara nchini Aisha Jumwa, mbunge wa eneo hilo Kenga Mupe vile vile mwenyekiti wa bodi ya hazina ya michezo, sanaa na maendeleo Wakili George Kithi, waliitaka serikali kuangazia masuala mbali mbali yanayowakumba wakaazi wa kilifi, ikiwemo uhaba wa maji safi, ukosefu wa dawa hospitalini na uvamizi wa ndovu kwa wakaazi wa eneo bunge la Ganze.
Awali naibu rais alitembelea miradi mbali mbali eneo hilo ikiwemo uzinduzi wa mradi wa nyumba za bei nafuu, na nyumba za malazi kwa wanafunzi wa taasisi ya ufundi, na ukaguzi wa mradi wa kituo cha huduma eneo la Shikaadabu huko Rabai.
Taarifa ya Joseph Jira

