News
KAA imemteua Moses Wekesa kuwa Mkurugenzi mkuu
Bodi ya usimamizi katika Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Kenya (KAA) imemteua Moses Wekesa kuwa Mkurugenzi mkuu mpya.
Uamuzi huu umefuatia mchakato mkali na wa ushindani wa usaili uliomtambua Wekesa kama kiongozi bora wa kuendesha ajenda kabambe ya KAA.
Wekesa amesimamia miradi ya hali ya juu katika sekta mbalimbali za uchumi barani Ulaya, Asia, Pasifiki na Afrika.
Hapo awali, alihudumu kama mkurugenzi wa maendeleo ya Biashara katika shirika la KenGen, ambapo aliongoza ukuaji wa shughuli kuu za kampuni.
Aidha, bodi inatambua mpito bora wa uongozi, hasa wakati juhudi za kisasa za mamlaka ya KAA za kuboresha viwanja vya ndege zinaendelea kuimarishwa ili kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa taifa.
KAA inaendelea kutekeleza mipango ya mageuzi, ikiwemo uboreshaji na upanuzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA), unaolenga kuimarisha nafasi ya Kenya kama kitovu cha kikanda cha usafiri wa anga na usafirishaji wa mizigo.
Taarifa ya Joseph Jira
News
EACC yafaulu kurejesha shilingi bilioni 7.8 zilizoporwa.
Tume ya maadili na kupambana na ufisadi EACC imesema imefaulu kurejesha shilingi bilioni 7.8 zilizoporwa.
EACC kwenye taarifa yake kwa vyombo vya habari, imeeleza kwamba fedha hizo zinajumuisha mali na raslimali za umma zilizopowa na baadhi ya wakenya wasiojali maslahi ya wengine na maendeleo ya taifa.
Tume hiyo ambayo ilitikwa jukumu la kukabili ufisadi na kuendeleza uadilifu kwa maafisa wa umma, mashirika na taasisi imekuwa ikifuatilia sakata mbalimbali za ubadhirifu wa mali ya umma ambao mara nyingi umekuw ukitekelezwa na baadhi ya wakenya ikiwemo viongozi wa kisiasa na maafisa wa idara mbalimbali za kiserikali.
Tume hiyo ya EACC ilifafanua kwamba kumekuwa na ongezeko la visa vya uporaji wa mali ya umma, ikisisitiza kwamba maafisa wa Tume hiyo wako makini kuhakikisha ufisadi nchini unakomeshwa.
Afisa mkuu mtendaji wa EACC Abdi Ahmed Mohamud, alisema kwamba viwango vya ufisadi nchini vingali juu na makachero wa EACC wamefanikiwa kukabiliana na visa vya ufisadi kwa asilimia 72 katika kipindi cha miaka miwili iliyopita.
Mohamud aliongeza kuwa tume hiyo imefanikiwa kurejesha shilingi bilioni 7.8 zilizokuwa zimeporwa katika kipindi cha miaka miwili, huku akiahidi kwamba mikakati zaidi imeekezwa kuhakikisha ufisadi unakomeshwa nchini.
“Juhudi tulizoweka katika kukabiliana na ufisadi nchini zimefaulu lakini kuna haja ya ushirikiano na washikadau
Wakati huo huo alieleza wasiwasi wake kuhusu kiwango cha hasara kilichorekodiwa katika miaka ya hivi karibuni akifichua kuwa takriban shilingi bilioni 10.74 zilipotea kupitia ufisadi katika kipindi chab miaka miwili pekee iliyopita.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Wakaazi watishia kuandamana kufuatia uhaba wa maji Kilifi
Wakaazi wa kaunti ya Kilifi wametishia kuandamana hadi katika ofisi za Gavana wa kaunti ya Kilifi Gideon Mung’aro kufuatia uhaba maji uliyodumu kwa takribani mwezi mmoja katika baadhi ya maeneo ya kaunti hiyo.
Wakaazi hao wakiongozwa na Kiongozi wa kidini wa Kanisa la Kibaptist kanda ya Pwani Rev. Francis Katana, walisema suala la maji ni muhimu kwa jamii za kaunti ya Kilifi na kwamba serikali ya kaunti inafaa kulichukuliwa kwa uzito suala hilo na kulitatua.
Katana anasema idadi kubwa ya wakaazi hasa wa mji wa Malindi wamekuwa wakipitia changamoto hiyo kwa mda mrefu na hata baada ya kuwasilisha lalama zao kwa idara husika ikiwemo ofisi za Kampuni ya usambazaji maji ya Malindi, MAWASCO, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa kukabiliana na changamoto hiyo.
Kiongozi huyo wa kidini alisisitiza kwamba maandamano hayo yatafanywa kwa kuzingatia amani na kwamba wakaazi watatembea hadi katika ofisi za Gavana Mung’aro ili kuwasilisha lalama zao.
“Tumechoka na hii shida ya uhaba wa maji iliyodumu kwa mwezi mmoja sasa na tutafanya maandamano hadi kwa ofisi za Gavana ili atueleza shida iko wapi, mbona wakaazi tunahangaika na uhaba wa maji”, alisema Rev. Katana.
Viongozi hao wa kidini pamoja na wakaazi wamelalamikia kutoangaziwa kwa maslahi yao licha ya kuwasilisha lalama kwa viongozi na wawakilishi wa maeneo yao, wakisema wakati umefika sasa kwa viongozi kuwajibika ama wananchi watatumia mamlaka yao ya kidemokrasia kuwatimua kazini.
Kwa upande wake Mwanasiasa Peter Ziro aliitaka serikali ya kaunti ya Kilifi kutatua changamoto hiyo mara moja ili kuwapungumzia mahangaiko wakaazi hao, akisema serikali ya kaunti iko na raslimali za kutosha za kuzikabili changamoto zinazowakumba wananchi mashinani.
“Tunashangaa na serikali hii ya Gavana Mung’aro, yani suala la maji ambalo ni uhai kwa wananchi waliyomchagua analichukulia kama jambo la mzaa, watu wanahitaji maji kwa matumizi ya kinyumbani na tukiendelea hivi basi tutateseka. Viongozi waliopewa jukumu la kushughulia maslahi ya wananchi ni lazima wawajibike kikamilifu”, alisema Ziro.
Akijubu lalama hizo zilizoibuliwa na wakaazi hao, Mkurugenzi wa Kampuni ya usambazaji maji ya Malindi, (MAWASCO) Felix Wanje alikiri kuwepo kwa changamoto hiyo, akisema ilichangiwa na kukatwa kwa nguvu za umeme kutokana na deni la umeme ambalo bado halijalipwa.
“Changamoto kweli ipo na hiyo shida tunaishughulikia na wananchi watapata maji hivi karibuni. Tatizo hilo lilichangiwa na kukatwa kwa nguvu za umeme kutokana na deni ambalo bado tunadaiwa lakini tunalishughulikia suala hilo”, alieleza Wanje.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

