News
Kaunti ya Kilifi yawaagiza wauguzi kusitisha mgomo na kurejea kazini
Huku mgomo wa wauguzi wa kaunti ya Kilifi ukiingia siku yake ya pili, na kusambaratisha utaoji wa huduma za afya, Serikali ya kaunti hiyo imejitokeza na kuzungumzia suala hilo.
Kati ya lalama zilizochangia Wauguzi kushiriki mgomo ni pamoja na malimbikizi ya mishahara ya mwezi Januari na Februari mwaka wa 2021, kutopandishwa vyeo, mazingira duni ya kazi miongoni mwa masuala mengine.
Msemaji wa serikali ya kaunti ya Kilifi Jonathan Mativo alisema japo serikali ya kaunti hiyo inafahamu kuhusu malimbikizi hayo ya mishahara ikiwemo malimbikizi ya deni la zaidi ya shilingi bilioni 11, kamati maalum imebuniwa kusawazisha suala hilo.
“Tunajua kuna malimbikizi ya deni la zaidi ya shilingi bilioni 11 lakini hiyo haihusiani na masuala haya ya mgomo wa wauguzi, ndiposa tunasema kuna jopo liliundwa kuangalia suala hilo la baada ya siku 45 litatoa ripoti yake”, alisema Mativo
Mativo, aliwarai wauguzi hao kurejea kazini na kushiriki mazungumzo ya kutatua matakwa yao ili kuhakikisha huduma za afya katika hospitali na zahanati za umma, hazikumbwi na changamoto.
“Tuna waagiza wauguzi wote walio katika mgomo kurejea kazini mara moja na kushiriki mazungumzo ya kutatua matakwa yao, tunajua kwamba kuna malimbikizi ya mishahara yao ya mwezi Januari na Februari mwaka wa 2021 lakini hiyo hatuaezilipa kwa sababu kuna kesi Mahakamani na Jaji Mbaru alitoa uamuzi wa wazi kabisa kuhusu suala hilo,” alisema Mativo.
Waziri wa Afya katika serikali ya kaunti ya Kilifi Peter Mwarogo alitoa onyo kali kwa Muungano wa wauguzi hao kwamba utachukuliwa hatua za kinidhimu iwapo utawashurutisha wauguzi watakaorejea kazini ama kukatiza huduma kwenye hospitali za kaunti.
“Taratibu za kupandisha wauguzi vyuo ziko na tunawaambia wauguzi warudi kazini na wale ambao wanaendelea na kazi hatutarusu watishie ama mtu kutatiza shughuli za hospitali, wale watapatikana tutawachukulia hatua na hata kuwafungulia mashtaka Mahakamani”, alifafanua Mwarogo.
Akizungumzia mgomo huo wa wauguzi, Mwenyekiti wa bodi ya huduma za umma kaunti ya Kilifi Albert Muturi alisema licha ya kufanya vikao kadhaa na Muungano wa wauguzi, na hata wauguzi 530 kupandishwa vyeo, hawafai kugoma.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Ethekon: Uchaguzi mkuu utakuwa huru, haki na uwazi
Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC imeanza rasmi zoezi la kuwasajili wapiga kura wapya kote nchini, huku ikilenga kuwasajili wapiga kura milioni 6.2, kabla ya uchaguzi mkuu ujao.
Mwenyekiti wa Tume hiyo Erastus Ethekon aliwahakikishia wakenya kwamba makamishna wa tume hiyo watahakikisha uchuguzi mkuu ujao unakuwa huru, haki na uwazi.
Akizungumza katika kaunti ya Kwale wakati wa kuzindua wa zoezi la usajili wa wakipiga kura kote nchini, Ethekon alisema serikali imewekeza raslimali za kutosha za kufanikisha zoezi hilo.
“Nataka kuwahakikishia wakenya kwamba tumejipanga kama IEBC na tuko na raslimali za kutosha kuhakikisha zoezi la usajili wa wapiga kura linaendeshwa vyema na uchaguzi mkuu utakuwa huru, haki na wazi ili kuhakikisha wakenya wanatekeleza jukumu lao la kidemokrasia na hatua hiyo tutafikia idadi ya wapiga kura zaidi ya milioni 27”, alisema Ethekon.
Naye Naibu Mwenyekiti wa IEBC Fahima Araphat alisema tayari maafisa wapya wa IEBC elfu 12 wameajiriwa kuhakikisha zoezi hilo liendeshwa vyema ili kusajili idadi kubwa ya wapiga kura
“Sisi tunafanya kazi yetu bila kuegemea upande wowote wa kisiasa na tuko tayari kuhakikisha anashinda uchaguzi anatangazwa mshindi kwa haki, na kama tuko na makarani elfu 12 na wote wasajili wapiga kura wapya elfu 10 kila moja tutakuwa na idadi kubwa ya wapiga kura, sasa hiyo ndio tunalenga kupata”, alisema Fahima.
Kwa upande wake Gavana wa kaunti ya Kwale Fatuma Achani, aliipongeza tume hiyo kwa zoezi hilo endelevu la wapiga kura, akisema ni hatua ya kipekee kwa jamii ambazo zimekosa fursa ya kujisajili kama wapiga kura.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
IEBC yasema idadi ya wanaojisajili ni ndogo mno
Zoezi endelevu la usajili wa wapiga kura kote nchini limeng’oa nanga huku maafisa wa Tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC wakilenga idadi kubwa ya vijana katika zoezi hilo.
Katika kaunti ya Kilifi eneo bunge la Kilifi Kazkazini, zoezi hilo limefanyika katika vituo vinne tofauti huku idadi ndogo ya wapiga kura ikishuhudiwa licha ya vuguvugu la TUKO KADI kuanzishwa na vijana ili kuwajisajili wapiga kura.
Akizungumza na Wanahabari wakati wa zoezi hilo, Naibu Afisa wa usajili wa wapiga kura katika eneo bunge la Kilifi Kazkazini Abdul Mohammed aliwarai vijana kujitokeza kwa wingi na kujisajili.
Mohammed pia aliwarai vijana kukoma kutumiwa vibaya na wanasiasa kwa manufaa yao binafsi, akipongeza vuguvugu lilionzishwa na vijana la TUKO KADI kama njia moja ya kuwahamasisha vijana kujisajili kama wapiga kura.
“Tumeanza zoezi hili na tunawahimiza vijana wajitokeze kwa wingi na kujisajili kama wapiga kura ili kutumia nafasi hiyo kuchagua viongozi wanawataka na wala wasikubali kutumiwa vibaya na wanasiasa”, alisema Mohammed.
Kwa upande wao baadhi ya vijana waliojisajili waliwarai vijana wenzao kujitokeza kwa wingi na kushiriki zoezi hilo ili kuchagua viongozi wanaohisi wataleta maendeleo sawa na kubuni nafasi za ajira.
Taarifa ya Elizabeth Mwende

