News
Mahakama Kuu yasitisha mpango wa Marekani na Kenya wa Karantini
Mahakama Kuu nchini imesitisha kwa muda mpango wa serikali ya Marekani na Kenya wa kuanzisha kituo cha karantini cha Ebola humu nchini.
Jaji wa Mahakama hiyo, Patricia Nyaundi, ameagiza kusitishwa kwa muda kwa utekelezaji wa makubaliano hayo hadi pale kesi iliyowasilishwa Mahakamani itakaposikilizwa na kuamuliwa.
Katika uamuzi wake, Jaji Nyaundi alisema Kenya pia hairuhusiwi kupokea mtu yeyote aliyekumbana na Ebola au aliyeambukizwa ugonjwa huo chini ya mpango huo hadi kesi hiyo itakapomalizika.
Shirika la kutetea haki za kiraia la Katiba Institute liliwasilisha kesi hiyo mahakamani likipinga mpango huo siku hiyo hiyo ulipotangazwa.
Shirika hilo limesema kuanzishwa kwa kituo hicho kwa siri na bila ushirikishwaji wa umma kunazua maswali mengi kuhusu haki za maisha, afya, uwajibikaji wa serikali na usimamizi wa bunge.
Kabla ya kesi hiyo kuwasilishwa Mahakamani, Serikali ya Marekani kupitia Rais Donald Trump ilikuwa imekubaliana na Kenya na kutangaza mpango wa kuwahifadhi kwa muda raia wake waliokumbana na virusi vya Ebola nchini Kenya.
Hatua hii ililenga kuzuia ugonjwa huo kuingia katika ardhi ya Marekani, ambapo sasa mpango huo umekumbana na kikwazo kikubwa baada ya Mahakama kuu nchini kusimamisha kwa muda mpango huo.
Kwa mujibu wa Ikulu ya White House, raia wa Marekani waliokuwa katika maeneo yenye mlipuko wa Ebola lakini hawajaonyesha dalili za ugonjwa huo walitarajiwa kuwekwa katika kituo maalum cha karantini katika Kambi ya Anga ya Laikipia mjini Nanyuki.
Maafisa wa utawala wa Marekani walikuwa wamesema wale ambao wangepata dalili za Ebola hawangerejeshwa Marekani, bali wangepelekwa katika nchi nyingine kwa matibabu ya juu zaidi.
Hatua hiyo ilionekana kuwa mabadiliko makubwa ya sera ikilinganishwa na milipuko ya Ebola iliyopita ambapo wagonjwa Wamarekani waliruhusiwa kurejeshwa nyumbani kwa matibabu.
Lengo la mpango huo lilikuwa kuhakikisha hakuna kisa cha Ebola kinachoingia nchini Marekani.
News
Baraza la Jamii ya Sekuye lalamikia uchimbaji wa madini kiholela
Baraza la Wazee wa jamii ya Sekuye eneo la Moyale kaunti ya Marsabit limejitokeza na kulalamikia kuharibiwa kwa mazingira ya maeneo yao hasa katika kijiji cha Dabel kutokana na uchimbaji madini kiholela.
Wazee hao wamewalaumu viongozi wao ikiwemo serikali ya kaunti kwa kulinyamazia suala hilo huku wakaazi wakiendelea kunyanyaswa raslimali zao.
Baraza hilo, chini ya Katibu wake mkuu Haji Hassan Tepo, limedai kwamba uchimbaji huo wa madini kiholela, unyakuzi wa ardhi, unyanyasaji wa jamii umechangiwa na baadhi ya wawekezaji kutoka taifa Jirani la Somalia na Ethiopia ambao hawana vibali halali.
Hassan aliimtaka serikali kupitia Waziri wa madini nchini Hassan Ali Joho kuingilia kati suala hilo na kuhakikisha uchumbaji wa madini katika kijiji cha Dabel unasitishwa kwani wawekezaji zaidi ya 20 wamebuni makundi na kuendelea kuwanyanyasa wenyeji.
Hassan aliweka wazi kwamba baraza hilo pamoja na jamii ya Sekuye linapinga mpango huo na kusisitisha kwamba hawatakubali ardhi yao wanayoitegemea kwa shughuli mbalimbali kutumika vibaya.
Naibu Mwenyekiti wa baraza hilo Abdukadir Dilo alisema hali hiyo imewasabibishia hasara kwani mifugo imeangamia, uchumi wa kijiji hicho ukididimia zaidi na akamtaka rais Ruto kuingilia kati kwani licha ya Waziri Murkomen kufunga uchumbaji kufuatia utovu wa usalama bado wawekezaji kutoka Ethiopia na Somali wamekuwa wakiendeleza mpango huo.
Wazee hao hata hivyo walisisitiza kwamba hawatakubali kuachilia ardhi yao kunyakuliwa na watu wanaodai kuwa wawekezaji ilhali vijana wa eneo hilo hawana kazi, huku wanafunzi wakiacha shule na zaidi ya akina mama 22 wakiachwa na wanaume zao kufuatia suala hilo katika kijiji cha Dabel.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Murkomen ahimiza ushirikiano wa pamoja na wadau wa masuala ya ubaharia
Waziri wa usalama wa ndani Kipchumba Murkomen, ametoa wito wa kuimarishwa kwa ushirikiano kati ya washirika na wadau ili kuimarisha usalama wa baharini na maziwa makuu.
Akizungumza wakati wa ufunguzi rasmi wa kongamano la kamati ya uongozi wa Jukwaa la ushirikiano wa taarifa ya kanda ya Indo-Pasifiki (IORIS) lililofanyika mjini Mombasa, Waziri huyo alisisitiza kuwa ushirikiano wa mapema ni muhimu katika kukabiliana na vitisho vinavyoibuka vya usalama wa baharini.
“Ushirikiano wa mapema na muhimu katika kulinda usalama wetu wa baharini,” alisema Murkomen.
Kongamano hilo la siku tatu linaandaliwa kwa pamoja na huduma ya Walinzi wa Pwani ya Kenya (KCGS) pamoja na mradi wa njia muhimu za baharini wa Indo-Pasifiki unaofadhiliwa na Umoja wa Ulaya (EU-CRIMARIO), ukiwaleta pamoja wadau wa usalama wa baharini..
Mradi wa EU-CRIMARIO umeundwa kuimarisha usalama na ulinzi wa baharini kupitia kuboreshwa kwa ushirikiano wa taarifa na uratibu wa operesheni.

Kongamano la siku tatu la kamati ya uongozi la Jukwaa la ushirikiano wa taarifa ya kanda ya Indo-Pasifiki (IORIS), Mombasa
Mpango wake mkuu, IORIS, ni jukwaa salama na lisiloegemea upande wowote linalotumia mtandao, unaounganisha zaidi ya mashirika 150 kutoka nchi 70, na kuwezesha uratibu wa operesheni za baharini kwa wakati halisi.
Kauli za Murkomen ilijiri kufuatia tangazo la Rais William Ruto kwamba kampuni ya usafiri wa baharini ya Norway, Wilhelmsen, itaajiri mabaharia 1,000 kutoka Kenya, baada ya mazungumzo na kampuni hiyo.
Hafla hiyo ilihudhuriwa na Mkurugenzi wa EU-CRIMARIO Martin Cauchi Inglott, Mkurugenzi mkuu wa huduma ya walinzi wa Pwani ya Kenya Bruno Shioso, Naibu mkuu wa ujumbe wa umoja wa Ulaya nchini Kenya Ondrej Simek, pamoja na washkadau wengine.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi

