News
Polisi watoa onyo kwa wanyakuzi wa ardhi Kilifi
Idara ya usalama kaunti ya Kilifi imetoa onyo kali kwa wanaoendeleza unyakuzi wa ardhi za umma, ikisema watakabiliwa kikamilifu.
Kamishna wa kaunti ya Kilifi David Wanyonyi ametoa onyo hilo, akizidi kulionya kundi la Team Mashamba dhidi ya tabia hiyo.
Katika kikao na Wanabahari kuhusu usalama wa kaunti ya Kilifi kabla ya ziara ya rais William Ruto ya uzinduzi wa miradi ya maendeleo, Wanyonyi amesema serikali haitalinyamazia suala hilo wakati wananchi wakiendelea kuhangaishwa.
Kamishna Wanyonyi alisema tayari maafisa wa usalama wako nyanjani kuhakikisha usalama unaimarishwa kabla ya ziara ya rais, akiwataka wananchi kuondoa wasiwasi kwani maafisa wa usalama wako imara kulinda mali na raslimali za wananchi.
“Kama maafisa wa usalama tunatoa onyo kwa wavamizi wa mashamba ya umma wakidhani hayatumiki, tunawaambia hiyo tabia waache, hasa hii Team Shamba imekuwa na tabia ya kuvamia mashamba na kugawa, tunawaambia hiyo tabia hatutakubali na kutawakamata”, alisema Wanyonyi.
Aidha alisisitiza kwamba maafisa wa usalama hawatarudi nyuma katika kupambana na walanguzi wa dawa za kulevya kaunti ya Kilifi, akisema watakamatwa na kufikishwa Mahakamani ili kulinda vijana dhidi ya Mihadarati.
“Ni kweli kumekuwa na kesi za Mihadarati, lakini tunasema kwamba kama maafisa wa usalama kwa ushirikiano na vitengo mbalimbali tutahakikisha walanguzi wa Mihadarati wamekamatwa na kufikisha Mahakamani kulingana na sheria’,alisisitiza Wanyonyi.
Ziara ya rais Ruto kanda ya Pwani inatarajiwa kuwa na manafaa makubwa kwa wananchi, huku suala tata la ardhi, likitarajiwa kuangaziwa na wananchi kupewa hati miliki.
News
Wadau wa sekta ya uchukuzi wasitisha mgomo wao
Maafisa wa sekta ya uchukuzi wameahirisha mgomo wao baada ya mazungumzo yaliyoongozwa na Rais William Ruto katika ikulu ya Mombasa.
Maafisa hao wakiongozwa na rais wa Muungano wa wamiliki wa matatu Albert Karagacha wamesema kuwa mengi ya masuala waliokuwa nayo ikiwemo kupanda kwa bei ya mafuta nchini yameangaziwa kwa kina na rais Ruto.
Karagacha amewataka wahudumu wa sekta ya uchukuzi wa umma pamoja na wamiliki wa magari ya uchukuzi wa mizigo kuhakikisha wanarudisha magari yao barabarani, akisema masuala waliowasilisha kwa rais yameangaziwa
Akizungumza mda mfupi baada ya kufanya kikao na rais William Ruto mjini Mombasa, Karagacha amesema serikali imekuwa kiangazia kwa kina masuala mbali mbali yanayohusu sekta ya uchukuzi nchini.
Aidha amesema iwapo bado serikali itakuwa inajikokota katika kufanikisha masuala waliojadiliana basi wataitisha mazungumzo zaidi na Wizara husika ili kuafikiwa kwa ajenda zao huku akisema japo suala la mzozo wa mafuta sio jambo la Kenya pekee lakini taifa inawajibu wa kusaidia wananchi wake.
Wakati huo huo Karagacha amewataka wakenya kutoingiza siasa katika suala la kupanda kwa bei ya mafuta nchini.
Taarifa ya Joseph Jira
News
Mshukiwa wa ulanguzi na usafirishaji wa watoto anyimwa dhamana
Mahakama ya Shanzu imemnyima dhamana mshukiwa wa ulanguzi wa watoto zaidi ya 20.
Mahakama imeagiza mshukiwa huyo kuzuiliwa rumande ili kuwawezesha maafisa wa polisi kukamilisha uchunguzi wao.
Mahakama imeelezwa kwamba mshukiwa huyo Almasi Rama Amos mwenye umri wa miaka 27 alikamatwa na maafisa wa upelelezi kutoka kitengo cha kupambana na ulanguzi wa binadamu na ulinzi wa watoto (AHTCPU) pamoja na maafisa wa idara ya upelelezi wa Jinai kutoka kaunti ya Mombasa.
Kukamatwa kwake kufuatia wiki kadhaa za uchunguzi kuhusu ripoti za unyanyasaji wa watoto zinazowalenga wasichana wadogo walio katika mazingira magumu.
Rama, anayetuhumiwa kwa kujihusisha na kundi linalodaiwa kuwa la ulanguzi wa watoto na dhulma za kingono na kufikishwa katika Mahakama ya Shanzu kufuatia operesheni ya kiusalama iliyoidhinishwa na maafisa hao.
Rama alipatikana katika mtaa wa Nguu Tatu eneo la Concordia katika kaunti ndogo ya Kisauni akiwa na watoto watatu wa kike.
Mahakama imeelezwa kuwa mshukiwa anadaiwa kuendesha “vituo vya uokoaji” katika kaunti za Mombasa na Kilifi kwa kujifanya kuwalea na kuwapa ushauri.
Kulingana na uchunguzi vituo hivyo vilikuwa vikitumika kama msingi wa dhulma za kingono na unyanyasaji wa watoto.
Alipokamatwa, mshukiwa aliwaongoza maafisa hadi kituo chengeni eneo la Ribe katika eneo bunge la Rabai, ambapo maafisa wa upelelezi waliwaokoa watoto 19 wa jinsia ya kike na kufikisha jumla ya waathiriwa waliookolewa kufikia ishirini na wawili (22).
Mbele ya Mahakama ya Shanzu tarehe 21 Mei, 2026, mshukiwa amekabiliwa na mfululizo wa mashtaka, ikiwemo unajisi, biashara ya watoto kwa madhumuni ya kuwadhulumu kingono pamoja na unyanyasaji wa watoto ambapo amekana mashtaka hayo.
Kesi hiyo imepangwa kutajwa Juni 8, 2026.
Taarifa ya Teclar Yeri

