News
Serikali yahimizwa kuwachunguza viongozi wa kidini wa itikadi potovu
Kutokana na kuongezeka kwa mafundisho ya itikadi potovu katika madhehebu mbalimbali nchini, sasa serikali imehimizwa kuanza kuwatathmini upya na kuwachunguza wachungaji wote nchini.
Aliyekuwa Mwakilishi wadi ya Gongoni kaunti ya Kilifi Albert Kiraga alitoa tahadhari kwa serikali, akisema ni lazima ilifikirie upya suala hilo kwani linatishia maisha ya jamii nyingi kutokana na matukio ya kutisha katika kijiji cha Kwa Binzaro kaunti ya Kilifi.
Kiraga alizitaka asasi za kiusalama pamoja na mamlaka zengine nchini kuanzisha mchakato mpya wa kuwachunguza wachungaji wote nchini iwapo stakabidhi zao za kidini zinaambatana na mafundisho wanayotoa kwa waumini wao.
Akizungumza na Wanahabari, Kiraga alisema tukio la hivi majuzi katika msitu wa Shakahola na kijiji cha Kwa Binzaro na sasa katika eneo la Kaloleni ambapo mtu mmoja aliyejiita Kasisi alionenkana akicheza densi juu ya mti huku waumini wakigaagaa kwenye matope wakiimba na kupiga makofi.
Kwa upande wake Mhubiri Dkt Dorcas Chebet Juma, ambaye pia ni Mhadhiri wa chuo kikuu cha Pwani alisisitiza umuhimu wa elimu ya dini miongoni mwa wachungaji na ujuzi wa kidini kwa waumini, akisema hatua hiyo itakomesha itikadi za kidini na mafunzo potovu.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

