News
Waziri Ruku, aunga mkono mswada tata wa kuzuia maandamano
Waziri wa utumishi wa umma nchini Geoffrey Ruku ameendelea kuunga mkono mswada tata wa kudhibiti mikutano na maandamano wa mwaka 2024.
Mswada huo, ambao kwa mara ya kwanza uliwasilishwa na Ruku wakati alipokuwa Mbunge wa Mbeere Kaskazini, umeibuka tena wakati huu ambapo maandamano yanayoongozwa na vijana wa kizazi cha Gen Z yanaendelea kushika kasi kote nchini.
Maandamano haya yameibua hisia kali huku vijana wakiibua masuala ya haki za binadamu, uwajibikaji wa serikali, na mustakabali wa taifa.
Waziri Ruku alitetea mswada huo, akisema kwamba mfumo wa sasa wa kisheria kuhusu mikutano na maandamano hauna nguvu za kutosha kudhibiti maandamano ya vurugu na ghasia kwani maandamano ambayo yamekuwa yakifanyika nchini yamekosa mwelekeo na uongozi thabaiti.
“Sheria ya umma ya mwaka 1952 ni ya zamani sana. Haikutungwa kwa ajili ya Kenya ya kidemokrasia na kwamba sheria mpya itanyamazisha wakenya kwa vurugu na kuwezesha maandamano ya amani, alisema Ruku.
Kulingana na Waziri huyo, mswada mpya unapendekeza kufutwa kwa sehemu ya 5 na 6 ya sheria ya agizo la umma na badala yake kuanzisha mfumo mpya wa kusimamia maandamano na mikutano ya hadhara.
Kwa mujibu wa mapendekezo ya sheria hiyo, waandamanaji watalazimika kutoa taarifa kwa polisi kati ya siku 3 hadi 14 kabla ya kufanyika kwa mkutano au maandamano yoyote.
Hata hivyo, wachanganuzi wa masuala ya kisiasa pamoja na Wanaharakati wa kutetea haki za kibinadamu wamekosoa vikali mswada huo, wakisema ni njama fiche ya kuzuia sauti za wananchi, hasa vijana wa kizazi cha Gen Z.
Wakosoaji hao walisema mswada huo mpya unaweza kuibua masharti magumu zaidi kwa umma kuandamana kwa amani na kwamba kuhatarisha haki ya msingi ya kujieleza na kukusanyika kwa amani.
Mswada huo unalenga kuchukua mkondo mpya baada ya Mwakilishi Kike kaunti ya Nairobi Esther Passaris kuwasilishwa mapendekezo mpya kuhusu mswada huo ambapo analenga kuzuia waandamanaji kuandamana katika maeneo yaliopigwa marufuku hasa bunge, Mahakama, ofisi kuu za umma na Ikulu pamoja na waandamanaji hao kuwa umbali wa mita 100 kutoka maeneo hayo.
Taarifa ya Mwahoka Mtsumi
News
Polisi wanachunguza tukio la wizi dhidi ya raia wa kigeni
Maafisa wa Polisi kaunti ya Mombasa wanachunguza tukio la wizi dhidi ya mtalii wa kigeni lililotokea katika eneo la Nyali
Kulingana na ripoti ya maafisa wa polisi, mtalii huyo mwenye umri wa miaka 51 ambaye ni raia wa Marekani, anadai kulaghaiwa na kisha kushambuliwa na kundi la wanaume aliyokutana nao muda mfupi kabla ya tukio.
Ripoti hiyo imeeleza kwamba mnamo mwezi Aprili 9 mwaka huu, raia huyo wa kigeni akiwa katika mkahawa mmoja eneo la Nyali jijini Mombasa, alikutana na mwanaume aliyejitambulisha kama Alex, ambaye alimshawishi kuelekea katika nyumba ya Airbnb iliyoko karibu na mkahawa huo.
Taarifa hiyo ilifafanua zaidi kwamba alipofika katika chumba hicho, alikumbana na wanaume wengine watano waliokuwa wakimsubiri ambapo mlango ulifungwa na kisha akashambuliwa na kulazimishwa kutoa pesa na vitu vya thamani.
Wahalifu hao walitoroka na mali mbalimbali ikiwemo simu ya rununu, kompyuta mpakato (laptop), fedha taslimu pamoja na fedha za kigeni na pia walifanikiwa kutoa pesa kutoka kwenye kadi zake za benki kwa njia ya udanganyifu.
Maafisa wa polisi kutoka Bamburi kwa kushirikiana na maafisa wa upelelezi wa DCI Nyali walifika eneo la tukio na kuanza uchunguzi, ingawa hadi sasa hakuna mtu aliyekamatwa wala mali iliyopatikana.
Kesi hiyo imewekwa chini ya uchunguzi zaidi huku juhudi zikiendelea kuwabaini na kuwakamata wahusika wa tukio hilo.
Taarifa ya Mwanahabari wetu
News
Polisi eneo la Likoni-Mombasa inachunguza kifo cha mwanamke
Idara ya usalama eneo la Likoni kaunti ya Mombasa imesema inachunguza kifo cha mwanamke mmoja aliyefariki katika mtaa wa senti kumi.
Mkuu wa polisi wa Likoni Joseph Mutungi alisema mwanamke huyo anadaiwa kupoteza maisha wakati wakiwa nyumbani kwa mwanamme anayesemekana kuwa mchumba wake.
Taarifa za awali ziliarifu kuwa marehemu alikuwa mgonjwa na anadaiwa alifika hospitalini kusaka matibabu japo hakupata huduma na kurejea nyumbani bila kutibiwa.
Inasemekana baadaye mchumba wake alioondoka kwenda kazini na kumwacha chini ya uangalizi wa mwanamke mwengine katika ploti hiyo.
Hali yake inadaiwa kuzorota na hatimaye kuaga dunia.
Maafisa wa usalama walisema wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha kifo hicho.
Mwili wa marehemu unahifadhiwa katika chumba cha kuhifadhi maiti katika hospitali ya Coast general kwa uchunguzi zaidi.
Taarifa ya Mwanahabari wetu

